SURA YA NNE
Kama kuna
wanawake ambao husimbua mioyo ya wanaume mara tu watokeapo mbele yao hata
wanaume hao wakajisahau na kuzisahau shughuli zao, basi ni dhahiri pia wapo
wanaume ambao huisumbua mioyo ya wanawake kwa kiwango kile kile. Na kama kweli
wapo, miongoni mwao yumo Joram Kiango. Hayo yalijidhihirisha baada ya Waridi
kumtia machoni Joram alipoingia chumbani.
Moyo wake
ulipoteza mapigo kwa sekunde kadhaa. Roho yake ilihisi kupaa nje ya mwili wake.
Kadhalika, damu ilimsisimka kiasi cha kumfanya ahisi ganzi mwili mzima. Hivyo,
hakuweza kuyaondoa macho yake juu ya umbo la Joram ambaye alimsogelea polepole.
Nusura wazimu umpande Waridi alipoona uso na tabasamu la Joram, lililotosha
kuwa tiba kwa maradhi yake. Maradhi aliyoamini kuwa hayangeweza kutibika.
Kwa bahati
mbaya, Waridi hakuwahi kupenda mwanaume katika maisha yake. Hivyo hakujua
mapenzi ni nini. Hakuwahi kuyaonja. Kama angejua, angefahamu nini kitatokea.
Badala yake alihisi maumivu moyoni na huzuni kubwa akilini mwake. Akanusurika
kutokwa na machozi. Hakujua nini kinamtokea. Isipokuwa kitu kimoja tu
alikifahamu, Joram hakuwa mtu wa kufa, Hakuona sababu ya kumwua, Asingeweza...
Tazama
alivyosimama mbele yake kwa upendo na utulivu kama malaika asiye na hatia.
Tazama anavyochekelea kwa furaha kama nuru, Mtazame. La, huyu kijana si mtu wa
kufa. Waridi akawa ameamua hivyo.
"Nadhani
mimi ni mgeni wako, mpenzi, Joram alisema tena, akinyoosha mkono wake kumgusa
Waridi kwenye bega lake la kuume.
Joram
alikuwa ameshangazwa na uzuri wa msicha huyu. Vipi wengine waumbwe kwa
upendeleo kiasi hiki wakati wengine wasitofautiane sana na vinyago? alijiuliza.
Mavazi mazuri ya msichana huyu pia yalimchanganya Joram; yalikuwa mavazi mapya
ya thamani kubwa, kisha ya kihuni kama yalivyondaliwa mahususi kwa ajili ya
kumtongoza! Hicho hakikumshangaza Joram, Lakini alishangazwa na uso mzuri wa
msichana huyu ukiwa katika dimbwi la majonzi, mashaka, hofu na msiba. Hilo
halikumshangaza hata kidogo.
"Ndio...ka...
karibu kaka", waridi alianza kusema huku akibabaika,
Joram
alimvuta mkono na kumwongoza hadi kitandani, ambako alimketisha kisha naye
akaketi kando yake huku akiendelea kuushika mkono wa Waridi.
"Nilikwambia
kuwa sauti yako ni tamu kama ilivyo sura yako? Naamini sikukosea. Ama kweli
umeumbika bibie. Ulimhonga nini muumba hata akakupendelea?"
Sauti ya
Joram, tabasamu lake likasindikiza kila neno, hali hiyo ikamfanya Waridi aanze
kuchangamka. Akasahau yote yaliyokuwa mbele yake na kujikuta kazama katika
maongezi na Joram. Katika kipindi hicho kifupi bila kujifahamu Waridi alijikuta
tayari akiwa ameufunua moyo wake wote kwa Joram, akimsimulia matatizo yake
yote. Alipotanabahi alikuwa akisema: "Najisikia kutoweka nje ya nchi
hii".
"Kwanini?".
Swahili hilo
lilimzindia Waridi. Hakujua yapi alikuwa tayari kuyatamka ambayo hayakustahili
kuiacha milki ya kinywa chake, Hofu ikamrejea. Akalikumbua jukumu lililokuwa
mbele yake: kumfanya kijana huyu kuwa marehemu. Ama ni yeye atajayefanywa
marehemu.
Hofu hiyo,
ilizidi baada ya Joram kuinuka na kuiendea meza iliyokuwa na chupa mbili za
pombe huku akisema: "Bia hii? Unaonaje nikianza kuimimina tumboni mwangu
ili kupoza joto la Dar es Salaam kabla hujanieleza sababu za kuniita hapa?
Siamini kwama kweli umeniita kwa ajili ya kunishukuru tu, yaani hilo likusukume
kunitafuta..."
"Usinywe
hiyo pombe", Waridi alifoka.
"Kwanini
mpenzi? Nilidhani umeiandaa kwa ajili yangu", Joram alifuatwa na tabasamu
la kukata na shoka.
Waridi
alikuwa akitetemeka. Lakini asingeweza kusahau maneno ya yule mtu katili Proper
alipomwambia: "Nitakuwa chumba cha pili... Ukishindwa tena nitakuua papa
hapa..." Waridi hakupenda kufa, lakini pia hakuwa tayari kumuona kijana
huyu asiye na hatia, afe. Afanye nini? Kwa kutojua la kufanya akaanza kulia.
Mikono ya Joram ilitua tena mabegani kwa Waridi akimfariji na kumkumbatia huku
akisema.
"Kama
hutaki ninywe hii bia ni wazi kwamba kuna zawadi kubwa na tamu zaidi ya bia
uliyoiandaa kwa ajili yangu. Kwa bahati mbaya nina mazoea ya kunywa pombe kabla
ya yote. Kwa maana hiyo niruhusu ninywe bia moja tafadhali".
"Usi..."
Waridi alijaribu kufoka tena. Joram alimzuia kwa kuuziba mdomo wake kwa kiganja
cha mkono wake huku akiweka kinywa chakr karibu na sikio la Waridi,
akamnong'oneza.
"Najua
kitakachotokea. Sinywi pombe hiyo. Acha nijifanye kama nakunywa ili nimpumbaze
huyu anayetaka kuniua. Nitakuomba wewe uwe msiri wangu. Mwache aamini kuwa
ameniua. Mwache kila mtu aamini kuwa nimekufa. Nataka kufahamu hawa
waliokusudia kuniua jambo gani wanakusudia kutenda".
waridi
aliduaa. "Ume... umewezaje kujua? aliuliza kwa kunong'ona.
"Niliwahi
kufika eneo hili mapema na kumsikia alivyokuwa akikuamru. Nawe pia lazima
ufahamu kuwa uko hatarini. Huyu ni mtu hatari. Mara tuu utakapotoka hapa,
toroka uende kokote asikoweza kukufikia. Sasa acha nijifanye nainywa pombe
yake". Joram akaongeza sauti kusema. "Glasi? Acha ninywe
kihuni".
Joram
aliifungua chumpa moja na kuingia nayo msalani ambako aliimimina nusu kwenye
tundu la choo, Akarudi na kuitua mezani huku akiendelea kuongea na Warid,
mazungumzo yao yalifanyika taratibu kwa sauti ya chini. Mara kadhaa Joram
alimshika waridi na kumtomasa hapa na pale kwa ajili ya kumtoa hofu.
"sasa
mpenzi sikia", aliongeza. "Ninaye mgeni ambaye atakuja ofisini kwangu
baada ya nusu saa kuanzia sasa. Baada ya kumalizana na mgeni huyo, leo kutwa
nzima nitakuwa huru. Waonaje niende ofisini mara moja na kurudi sasa hivi?
Naamini leo tutashinda pamoja kwa furaha sana. Naamini itakuwa siku njema
twetu".
"Sawa",
Waridi alijikongoja kujibu.
"Tafadhali
nikukute, ukiwa kama ulivyozaliwa. Ikiwezekana, kitandani, sawa?"
"Bila
shaka".
Mara tu
Joram alipotoweka machoni mwake, Waridi alijikuta akirejewa na hofu. Ile hakika
na ushujaa ambao alikuwa ameuhisi kwa kusikia sauti ya Joram na kuyaona macho
yake yang'aavyo sasa ilikuwa kama ndoto tu. Ndoto ya kale. Hakujua lipi afanye.
Akaendelea kuduwaa kimya, akitazama huku na huku kama aliyetegemea kumwona
Zibril akimjia kwa lengo ka kutwa roho yake.
Waridi
angetimua mbio Proper alivyoingia ghafla huku akimtazama Waridi kwa macho ya
kutisha. Waridi angeweza kukimbia kama ukuta usingekuwa umemtenga na dunia ya
nje. Alichofanya ni kurudi nyuma hatua kadhaa hadi alipoegemea ukuta, macho
yenye hofu kayatoa kama kondoo aliyekuwa juu ya madhabahu, akisubiri kutolewa
kafara.
"Mwanakharamu...
malaya mkubwa, mwana wa malaya mkubwa...", Proper alifoka. "Umekosa
walau ushujaa wa kunidanganya kuwa hawara yako amekunywa pombe niliyomwandalia?
Mara hii umesahau kuwa mmekubaliana naye adai kuwa ameinywa ili asingizie kuwa
kafa. Nakusikitikia Bi. mdogo. Namsikitikia pia huyo hawara yako. Hajui
afanyalo. Anadhani kuwa anacheza na watoto wadogo kama alivyozowea. Nilikuwa
nimemfanyia hisani kubwa ili afe kistaarabu hakutaka. Kajitia ujanja. Sasa
atakufa kifo cha kusikitisha zaidi".
Jodor Proper
aligeuka kama anataka kutoka. Mara kama aliyekumbuka jambo alimgeukia tena
Waridi na kusema. "Nawe malaya mwovu hufai kuishi zaidi. Huna faida
duniani wala haki ya kuishi tena. Utamfuata mpenzi wako Bomba akhera. Mpe
salamu zangu, mwambie hongera kwa hila zake zisizo na ila". Akageuka na
kutoka.
Machozi
yalikuwa yamenyauka machoni mwa Waridi. Sasa aliiona dunia kama kitu ambacho
kilikuwa kando yake. Naam, maisha yake yalikuwa ukingoni. Asingeweza kutilia
mashaka sauti ile ya Proper yenye uhakika. Sauti ambayo masikioni mwake ilikuwa
kama saut ya mauti yenyewe.
Kwanini
aendelee kusubiri? alijiuliza. Kwanini asubiri kifo cha mateso na kashfa?
Akajiuliza kwanini asitangulie? Sasa macho yake yalikuwa yakitambaa kila mahali
kutafuta silaha yoyote ambayo ingefaa kumtoa roho. Mara macho ya waridi yakatua
kwenye ile chupa yenye pombe yenye sumu iliyoandaliwa kwa ajili ya Joram, bila
kufikiri kwa mara ya pili aliiendea ile chupa yenye pombe akajimiminia tumboni
mwake.
Mara Waridi
akapata faraja kubwa ambayo ilimfanya asahau hofu na kudharau vitisho vyote vilivyokuwa
mbele yake. Alijiona yu njiani hatua chache tu kufika katika milki mpya. Milki
ambayo itampa uhuru kamili.
Furaha hiyo
ikamuongoza Waridi, alitoka ndani ya chumba hicho na kuiendea lifti. Akatelemka
hadi chini. Aliiacha hoteli na kuanza safari ya kuelekea kituo cha mabasi.
Mavazi yake yakiwa kama yalivyokuwa, umbo lake likiwa kama lilivyo, na sura
yake nzuri ikiwa imepambwa na tabasamu, viliyafanya macho ya wanaume kumtazama
kwa mshangao wenye tamaa. Baadhi waliguna walipomuona, wawili walimkonyeza na
mmoja alidiriki hata kumfuata. Wote walipata tuzo kwa tamaa zao. Tuzo ambalo
lilikuwa tabasamu pana zaidi ambalo liliwafanya wabaki wameduwaa nyuma yake hoi
bin taabani.
Waridi
akaendelea na safari yake. Mwendo wake ukiwa nyongeza nyingine ya maneno kwa
watazamaji. Akiwa kajaza nyuma, kakatika kati na kunyooka alivyonyokeana,
ilikuwa kana kwamba hatembei bali anafanya maonyesho ya miondoko kama
wanavyofanya warembo katika mashindano ya miss. Mwenyewe akiwa hana habari
hizo, aliendelea na msafara wake hadi alipokifikia kituo na kujiunga na umati
wa watu waliokuwa wakisubiri usafiri wa umma.
"Gari
hii hapa dada", mtu mmoja alimwambia Waridi. Ilikuwa teksi. Waridi
hakufanya hiana, akajitosa ndani ya teksi hiyo huku akisema. "Nipeleke
Mburahati",
"Vizuri,
lakini waonaje kama tukipitia hapa Embassy Hoteli tukapate walau bia mbili
mbili baridi?", dereva alitupa ndoano yake.
"Samahani,
leo nina haraka, nitafute siku nyingine".
"Kesho".
"Sawa..."
waridi alilaghai. Rohoni akiamini kuwa kesho hatakuwa Dar es Salaam. Hatakuwepo
hapa nchini, wala popote Afrika. Atakuwa nje. Nje ya dunia. Aliendelea kuwaza
kwa furaha huku akimwitikia dereva huyo, "Ndio", kwa kila dereva huyo
alilosema wakati hata hamsikii. Walipofika mbele yavijumba vayo, Waridi alimtaka
dereva asimame. "Ni hapa, asante kaka", dereva hakuyaamini masikio
yake, "Yaani uaishi hapa. Katika vijumba hivi? Na unaishi hapa
dada?", dereva alishawishika kuuliza.
"Hapa
ndio kwangu", Waridi alijibu wakati akitelemka kutoka ndani ya gari.
"Hapa?",
dereva aliuliza tena kwa mshangao. Hakutia neno lingine. Badala yake aligeuza
gari lake na kurudi alikotoka kwa mwendo wa kasi.
Walidi
akapokelewa na wenzake waliojawa na mshangao. "Iwe", alisema mmoja
wao. "Ulikuwa wapi".
"Na
ilitokea nini hata ukaondoka bila kuaga?", alihiji mwingine. Maswali
yalikuwa mengi mno. Waridi hakuwa na muda wa kuyajibu yote. Wala hakukumbuka
ajibu maswali gani. Alichokumbuka ni jinsi alivyoingia chumbani kwake na
kujilaza kitandani akisubiri kifo. Usingizi mzito ukamchukua.
Alipoamka
ilikuwa usiku wa saa tatu. Chumba cha pili kitanda cha mwenzake kilikuwa
kikilalamika kwa uzito wa viumbe waliokuwa wakikitumia. Naye alikuwa akigongewa
mlango. Mteja akainuka na kumwendea. Alikuwa mtu mwenye umbo la mwili wa mtoto
na uso wa mzee. Alikuwa na pesa zake mkononi tayari. "Leo sifanyi
kazi", Waridi alimwambia mteja huyo na kufunga mlango wake. Hakujali
malalamiko ya mteja huyo. Alikuja mwingine. Na mwingine tena. Wote Waridi
aliwakatalia. Nao wakaondoka shingo upande.
Halafu akaja
huyu mteja ambaye hakukubali kuondoka. Alikuwa kavaa kofia kubwa iliyofunika
uso wake na koti kubwa lililofunika hadi miguuni. Aliingia kwa kujlazimisha na
kufunga mlango nyuma yake huku akisema, "Lazima".
"Leo
sitaki".
"Hata
kwa bei kubwa?".
"Hata
ukitoa milioni".
Mtu huyo
alicheka kidogo. "Mimi wanitaka. Umekuwa ukinisumbua muda wote huu",
Alitupa koti lake chini na kubaki katika suruali na shati. Akaivua kofia yake
na kuitupa juu ya koti. Ni hapo Waridi alipomtambua. Macho yenye hofu kubwa
yakamtoka.
"Bila
shaka utakuwa umenikumbuka ", alisema polepole. "Unadhani nilikusudia
ufe kistaarabu kwa ile sumu?, Ile ilikuwa maalumu kwa ajili ya Joram Kiango
peke yake. Wewe ni mwovu mwenye dhambi nyingi. Unastahili kufa kishenzi".
Kabla Waridi
hajafahamu kama ilimpasa kufanya nini, alijikuta tayari kadakwa ghafla kwa
mkono kwa mkono wenye nguvu, ambao uliibana mikono yake yote miwili. Haraka
kamba zikapita mikononi mwake. Alipotanabahi kupiga kelele, alijikuta katupiwa
dude fulani kinywani ambalo lilimziba kinywa. Mara akatupwa chini na kudungwa
sindano ambayo ilimlegeza hata asiweze kutapatapa.
Kisha kisu
kikali kilichomolewa kutoka ubavuni na kuanza kupita juu ya mwili wake. Maumivu
yalikuwa makali ajabu, lakini hakuwa na uwezo wa kulalamika. Alichoweza kufanya
ni kuendeleo kukodoa macho yenye dalili zote za hofu na maumivu. Macho hayo
yalishuhudia mikono yake ikikatwa mmoja baada ya mwingine na kuwekwa juu ya
kitanda. Kisha tumbo la waridi likafumuliwa na utumbo kumiminika katika sinia
lililokuwa mezani. Baada ya sekunde kadhaa alikuwa tayari amekata roho pindi
kichwa chake kilipokatwa na kuwekwa juu ya debe, kando ya kitanda.
Baada ya
kuridhika na kazi yake. Proper alizivua nguo zake zenye damu na kuzifunika
katika mifuko ya koti lake ambalo alilivaa na kisha kutoroka zake nje polepole
kama wateja wengine. Hapo nje aliwakuta wateja kadhaa ambao walisimama kwa
namna ya mstari wakisubiri zamu zao. Akafanya haraka kuiendea sehemu aliyoficha
gari yake.
Mteja
aliyeingia baada ya Proper aliduwaa kwa kutokumuona Waridi. Kisha alishangaa
kuiona mikono ya mwanamke huyo iliyolala peke yake juu ya kitanda. Halafu
akakiona kichwa kilicholowa damu, kimelala chali. Hakuyaamini macho yake. Na
ilipomtokea kuamini alihisi akili yake ikipaa. Alipiga kelele kwa nguvu na
kuanza mbio akielekea barabarani, Alianguuka, akainuka na kuendelea kukimbia.
Mtewa
mwingine alichungulia tu na kugeuka akianza safari ya kurudi zake alikotoka
kimya kimya.
Ni mteja wa
tatu aliyetoa taarifa kwa majirani na wenzake kuhusu kilichomtokea Waridi. Yeye
pia alitoweka. Majirani walichanganyikiwa kwa muda mrefu. Mmoja wao alitapika.
Wawili wakalia kwa nguvu. Umati mkubwa wa watu ulifika. Polisi pia
hawakuchelewa.
ITAENDELEA 0784296253
Comments
Post a Comment