KUFA NA KUPONA

SURA YA PILI

Wasiwasi

Sammy alikuwa ameelezwa kwa kifupi na Chifu juu ya habari yote, hivyo aliomba nimweleze kwa urefu mambo yalivyo. Wakati wote huo hata Sammy, hakuwa akiona dalili yoyote ya kupata mwangaza wa jambo hili. Wote tulionekana vibuda.

Hapo uwanja wa ndege palikuwa na ukaguzi mkali sana. Lakini kwetu siye Chifu alikuwa amefanya mipango yote, kwa hiyo tulipita moja kwa moja mpaka kwenye ndege. Wakati huo nilikuwa bado najaribu kufikiri jambo hili na lile, kama naweza kutoa jambo kamili lakini wapi. Yule mtu mwenye shuka na miwani myeusi alikuwa akija kwenye mawazo yangu kila wakati. Mambo niliyofikiria kwenye lile jengo lililobomolewa pia yalikuwa yakinijia mara kwa mara. Nikamweleza Sammy kila fununu, au jambo lolote nililofikiria linaweza kutusaidia. Sammy naye akanipa mawazo yake.

Ilipofika saa tatu u nusu ndege iliondoka. Tuliiangalia Dar es Salaam kama kwamba hatutaiona tena. Hakuna aliyeamini ataiona tena. Wasafiri wenzetu walionekana kuwa wachovu wote kama sisi tulivyokuwa, kwani kama unavyojua ni Jumapili asubuhi. Mie nadhani ndiye niliyekuwa mchovu kushinda wote. Kwa hiyo nilimwambia Sammy awe macho wakati mimi nikijipumzisha kidogo maana katika kazi yetu hii huwezi kujua ni nani adui na nani rafiki. Wote ni maadui zetu mpaka tutakapohakikisha wenyewe mia kwa mia, ni nani rafiki yako. Na pia nilimweleza kama kukitokea kitu chochote ambacho atakishuku aniambie. Kwani nilijua mchana huo Nairobi kungekuwa na shughuli kubwa sana.

Sammy aliponiamsha niliona kuwa tulikuwa tayari tumefika kwenye kiwanja cha ndenge cha Embakasi. Tulitelemka kwenye ndege. Kisha tulitafuta gari la kukodi twende zetu mjini. Sammy alinunua gazeti la "Sanday Nation" aone kama kuna kitu chochote juu ya tukio hili lakini hakukuwa na lolote, ila mambo mengi juu ya maonyesho ya mavazi na mashindano ya muziki mjini Nairobi. Tulikuwa tumemweleza Chifu asiruhusu hili jambo kuchapishwa mpaka Jumatatu wakati tutakapokuwa tayari tumeanza kazi yetu huko Nairobi.

Tulitazama huko na huko ili tupate gari gani tukodi. Tangu tutoke kwenye ndenge ulikuwa umepita muda wa robo saa na ushee hivi. Nia ya kungojangoja hapo kiwanjani ni kutaka kuona kama kuna watu wowote ambao walikuwa wanategemea kurejea kwetu, kwani siye kushuku kila mtu ndiyo kawaida yetu.

Tulipoona hakuna lolote, tulikodi gari moja la"Archers Tours." Tukamweleza dereva atupeleke mpaka Embassy Hoteli, ambako nduko tulitegemea kulala. Lakini Sammy hakuonelea vizuri wote kukaa katika Hoteli moja kwa hiyo yeye alitaka tumtelemshe Hoteli Pigalle. Tulipanga tuonane mara moja Hoteli Fransae, kusudi tupate kuonana na John Mullunga, kama ilivyopangwa.

Mimi nilishuka Embassy Hoteli, nikaenda katika ofisi yao, ambako nilijiandikisha kama Joe Masanja. Halafu huyo binti ambaye ndiye karani hapo Hotelini akanipa cheti changu, funguo na nambari za chumba. Nikaingia chumbani. Kilikuwa chumba kizuri maana kilikuwa kwenye pembe ya nyumba. Kilikuwa na madirisha mawili. Dirisha moja kwenye upande wa mtaa wa Koinange na moja lilikuwa limezibwazibwa na nyumba zingine. Baada ya kuweka vitu vyangu nilitelemka mara moja kwenda zangu Hotelini Fransae. Nilipopita pale ofisini, nikamweleza mshughulikaji wa simu kuwa kukija simu yangu achukue hiyo habari. Halafu nikampa shilingi ishirini. Akanitazama kwa macho ya kusema asante mara mia. Kwani tarehe ishirini kwenye jiji kama Nairobi, ni mwambo mbaya sana.

Kisha nikaharakisha kwenda zangu Fransae. Nilipofika mlangoni, nilimuona Sammy naye anamaliza kuingia. Nilimuona John amekaa kwenye pembe ya mlango upande wa kushoto kama ukiwa unaingia tu hotelini. Sammy alikuwa hamjui John, kwa hiyo yeye alikuwa bado anaendelea kwenye kaunta ya hoteli. Nilipoingia nilimpigia mluzi akageuka tukamfuata John pale pembeni. Tumewahi kufanya kazi na John huko Kampala, wakati tulipotumwa kuwatafuta waibaji almasi. Na ninakwambia wewe msomaji John kusema kweli si mchezo. Katika kila kesi wanayomweka John hawa watu wa Uganda jua kuna makubwa. John alikuwa amekaa na kijana mwingine mwenye sura ya kupendeza sana. Nafikiri John alimfanya rafiki yake kusudi huyo kijana awe anamtengenezea mpango kwa ndasa, kwani alidhani kuna msichana yeyote ambaye asingesimama kama huyo rafiki wa John akimpigia mluzi.

Tulipofika hapo John alitukaribisha tukae. Kisha akatufahamisha kwa rafiki yake ambaye anaitwa Robin Mwangi, Kikazi akiwa ofisa wa usalama nchini Kenya. Nayo Serikali ya Kenya ilikuwa imemleta Robin kwenye kazi hii. Mimi nilijifahamisha kama Joe Masanja, na Sammy kama Athumani Hassani. Na mikamfahamisha John kwa Sammy kama Fred Kamau. John tayari alikuwa amepata habari zote za kuja kwetu, na jinsi ambavyo Chifu alivyomweleza kama angeweza kumtambua Sammy, kwa kule kuwa na kamera shingoni. Wote tayari tulikuwa tumeshaelezana majina ambayo tutatumia. John alituagizia vinywaji. Aliagizia "Marteli Cognac" toti nane, pamoja na soda kwenye barafu.
  
Wakati tukinywa, John alitueleza, "Hapa tulipo si mahali pazuri sana kwa kuelezana habari, kwa maana watu wengi huwa wanakuja kuzimua hapa hotelini saa kama hizi, siku za Jumapili. Hata hivyo nitawatolea muhtasari wa habari niliyokwishapata," Alinyamaza, kisha akaanza kusema, "Joe kusema kweli tukio hili linatisha kuzidi matukio yote, kwani inaonekana wote tuko gizani kabisa. Miye nilidhani nitapata jambo lolote la maana lakini wapi. Robin nilimweleza mnamo saa moja aweke vijana wake mahali fulani kusudi huenda wakaweza kutupatia maelezo yoyote ama kama wanaweza kupata fununu yoyote. Lakini ajabu ni kwamba vijana wanne wameisha uawa katika muda huu wa saa mbili. Hii inaonyesha tutakuwa na muda mgumu sana, tena sana. 

"Mmoja alikuwa amepigwa risasi huko Embakasi. Mwingine ametiwa kisu huko "Uhuru Park". Wengine wawili walikutwa wameuawa huko Lavington Green kwa risasi. Sasa hata hatuwezi kuunganisha vifo hivi, ila tu kwamba watu hawa wako kila mahali. Na linaonekana kuwa kundi kubwa sana. Lakini jambo kubwa ni kwamba lazima tufanye kichwa cha tukio hilo.

"Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa kwenu amenieleza kwa simu anavofikiria. Nami ninakubaliana naye, kwani huyu mzee akibashiri kitu, naamini ni hivyo. Kwa hiyo sisi itatubidi tuendelee kama alivyofikiri, la sivyo tumekwisha". 

Bado mimi nilikuwa sijaweza kuunganisha jambo lolote. Ilikuwa bado ajabu. Ajabu kubwa. Hapo nilimwuliza John, "Unafikiri, sasa tutaanzia wapi?"

"Mimi nafikiri tutaonana usiku huko Starlight Klabu maana, yule kijana aliyekutwa Uhuru Park, alikuwa sehemu hizo. Na miye nilipochunguza sana ilionekana kama kwamba huyu mtu aliuawa katika nyumba fulani halafu akatupwa Uhuru Park. Kama unavyojua leo ni Jumapili watu wengi walikuwa bado wamelala.

Baada ya kukaguakagua afisa mmoja wa polisi alisema aliona tone la damu kwenye mlango wa Klabu hiyo. Nikaonelea vizuri nimwambie Mkurugenzi wa Usalama wa hapa amueleze Mkuu wa Polisi. Niliwataka wasiulize jambo lolote, au wasiulize maswali yoyote juu ya vifo hivyo mpaka baadaye. Kwa hiyo sasa tutatawanyika halafu tutaonana usiku huko Klabu. Wakati huu Robin na mimi tutaendelea kukusanya habari chache chache toka kwa maafisa wake. Nendeni mkapumzike.

Tuliagana na Robin akanieleza, "Kama ukitaka msaada wowote wa watu waweza kupiga ripoti ofisini kwetu, Chifu huko Dar es Salaam tayari amefanya kila mpango na wakubwa wa usalama katika nchi zote tatu za Afrika ya Mashariki."

Tulikubaliana kuwa wote tutaonana Starlight Klabu mnamo saa tatu usiku. Sammy alienda hotelini kwake, nami nikarudi hotelini kwangu kupumzika kidogo.

Nilipoingia hotelini kwangu nikaenda mpaka kwa mshughulikaji na simu kumwuliza kama amepata simu yoyote. Naye akasema kwamba alikuwa bado hajapata. Nilienda moja kwa moja kitandani kwangu nikalale.

Nilipoamka ilikuwa saa kumi na mbili za jioni. Nilioga na kunyoa ndevu. Halafu nikajitayarisha kwa kila njia ili niweze kuonekana kama mwandishi kweli kweli. Halafu nikaagiza chakula. Sikula chakula kizito sababu hali yangu haikuwa nzuri sana. Baada ya kula nilimpigia simu Sammy anipitie mnamo saa mbili na nusu.

Ilipofika saa mbili na nusu Sammy alinikuta baa ya Fransae. Tukafunga safari kwenda Starlight. Mimi nilitaka tuchukue taxi, lakini Sammy alikataa, kwa kusema, "Twende kwa mguu, maana tunaweza tukapata jambo la kufurahisha. Pia ni lazima uchukue bastola yako, maana kunaweza kuwa na mambo ya hatari."

Nilirudi chumbani kwangu, nikaweka bastola yangu ndani ya mkoba wake wa begani. Nikaweka koti langu juu nikafunga tai sababu mwezi wa saba, ni baridi sana Nairobi. Ningekuwa sehemu za Dar es salaam, wakati huo ningekuwa ninavaa furana. Kweli nilipojiona kwenye kioo nilionekana mwungwana. Na ninakwambia ninapokuwa nimevaa koti, huwezi kujua kuwa hata siku moja nimewahi kugusa bunduki. Nilirudi huko, baa kumpitia Sammy ili twende zetu.

Tulienda na mtaa wa Koinange, halafu tulipofika New Avenue Hoteli, tukashika Kenyatta Avenue. Tuliendelea na Kenyatta Avenue mpaka tuliposhika Uhuru Highway, tulikoingia katika kijinjia kinachopitia Uhuru Park. Tuliangaza huku na huko katika Uhuru Park lakini ilionekana hapakuwa na watu. Nadhani watu walikuwa wameishasikia kifo cha huyo kijana. Pia tulitegemea kuwa kama watu hao wamekuwa wakifuata myenendo yetu, huenda wakawa wanatufuata. Hivyo Sammy akawa tayari tayari na visu vyake ikiwa kutatokea matata. Lakini hatukupata jambo lolote.

Tulipoachana na Uhuru Park, tulishika Kirk Road. Tukaenda zetu moja kwa moja mpaka Starlight. Nje ya Klabu hiyo tulikuta watu wengi wakikata tikiti. Wanawake walikuwa wengi sana hapo nje, na walionekana wakitafuta wanaume wa kuwaingiza ndani. Lakini sisi tulikata shauri tusiwajali maana wangeweza kuingilia kazi yetu. Nilienda nikakata tikiti halafu tukaingia ndani.

Hii Starlight Klabu inapendeza mno maana hali ya hewa ya humo ndani ni tulivu kabisa. Kila mtu alionekana ni Mwungwana. Watu wengi walikuwa wameishaingia. Wengi wao walikuwa wawili wawili, yaani" Kitu Mtu." Nadhani unanielewa ninaposema hivyo. Tulienda tukakaa kwenye pembe moja ya kulia karibu na mlango mkubwa wa kuingilia. John alikuwa bado hajafika. Tulishangaa sana, lakini tulijua tu ya kwamba atafika muda si mrefu. Punde si punde Robin alifika. Na mara alipotuona akatufuata.

Robin aliuliza, "Fred yuko wapi?"

"Hata siye bado hatujamuona. Tulidhani mngefika wote hapa, "alijibu.

"Hata, aliniambia kuwa yeye atakuwa hapa mnamo saa mbili u nusu, kama ni hivyo basi huenda yuko kwenye ile baa ya nje, au amepata habari fulani ambayo anaishughulikia."

Kisha Robin aliondoka akaenda kwenye baa ya nje kuchunguza kama Fred yuko huko. Aliporudi alitueleza kwamba Fred hakuweko. Sammy aliagiza vinywaji. Muziki nao ulianza kupigwa na vijana wa Fiesta Matata ambao hupiga muziki taratibu kabisa. Wakati huo wote tulikuwa tukimngojea Fred lakini hakuonekana. Tulianza kupatwa na wasiwasi mwingi sana. "Kwani Fred anaishi wapi?" Sammy alimwuliza Robin.

"Anaishi Princess Hoteli."

"Afadhali nikampigie simu huenda anaumwa," nilisema 

"Sammy uwe unaangalia kama yuko mtu mwenye shauku na mimi nipigapo simu."

Nilipopiga simu hotelini kwa Fred ilionekana hayuko kwani kengele iliendelea kulia kwa muda mrefu sana. Nilikata simu na kurudi pale kwa akina Sammy. Niliporudi Sammy alinieleza, "Ulipokuwa ukienda msichana mmoja ambaye alikuwa amevaa mini alikuwa akikuangalia kwa jicho la pembeni pembeni. Msichana huyo alikuwa akicheza dansi na kijana fulani. Halafu alipokuona ukienda kwenye simu alisogea mpaka kwenye kiti cha karibu na simu, kisha akajifanya kuwa anasoma gazeti. Na baadaye msichana huyo akapotea mumu humu mwenye watu."

Hilo jambo niliona huenda ni hatua moja wapo. Lakini hatua hii ilikuwa bado haina uhusiano wowote na tukio letu. huenda ni kwa sababu ameona ajabu kwa nini tulipiga simu, na kwamba tulikuwa tumekaa tu bila wanawake na hali tunaonekana vijana nadhifu mno.

"Habari zenu," sauti nyororo ilitoka kwa nyuma yetu. Kila mtu kati yetu alipatwa na kigugumizi cha kujibu, kwani wote tulipotupa macho nyuma yetu, tulimwona msichana mzuri mmno!

Nakwambia maishani mwangu nimeona wasichana, lakini ilivyo ni kuwa huyu msichana alishinda. Nilisikia nywele zikinisimama nilipomwangalia tena. Nilijikaza kisabuni nikamjibu, "Siye wazima tu, vipi wewe?"

"Miye salama tu. Nilidhani kuwa huenda nyiye ni wageni hapa. Na kwamba huenda mlipofika hapa mlifanya mpango na wasichana fulani fulani mwonane nao, lakini hawajaonekana, si hivyo?"

"Kidogo huenda uko sawa, lakini si sana,"nilimjibu.

"Mbona unaonekana mwenye wasiwasi basi? Nilidhani kwamba ulienda kupiga simu kwa madhumuni ya hao wasichana." Akanyamaza hali akinitazama machoni.

Kweli mimi nakwambia sitaki wasichana wanaonitazama machoni. Kwa hivyo msichana huyu mara moja alinitisha. Macho yake yalionekana kusinziasinzia, lakini yanaweza kukusoma moyoni mwako.

"Nilikuwa napiga simu kwa rafiki yangu mmoja ambaye ni mwandishi juu ya mambo ya muziki. Yeye tulimwacha Acadia Klabu. Nilitaka kumweleza aje huku kwani, muziki wa hapa unaonyesha umeshinda. Lakini inaonekana kuwa muziki wa huko umewaingia sana hata hawasikii mlio wa simu," niliongopa.

Alitabasamu. Tabasamu hilo lilifanya nywele zangu zisimame tena.

"Kweli nimeupenda muziki wa hapa," alisema msichana huyo. "Hata mimi huwa napenda bendi hii hii, na mahali papa hapa."

"Jina lako nani, "aliulizwa na Sammy.

"Mimi naitwa Lulu. Lulu Jack, kazi yangu ni kuonyesha mavazi. Nimetoka Kampala kuja kwenye maonyesho ya mavazi hapa Nairobi ambayo yatachukua kama wiki mbili hivi." Alinyamaza kwa muda wa kupisha mate yapite kooni. Kisha akauliza," Na nyiye ni akina nani?"

"Miye ni Athumani Hassani, na huyu," alisema Sammy akionyesha kidole kwangu," ni Joe Masanja. Na huyo ni Robin Mwangi. Kazi yetu sisi ni uandishi wa habari juu ya maonyesho ya mavazi. Hata sisi tumeletwa na yaya haya maonyesho ya mavazi. Hivyo inaonyesha tutaonana mara nyingi toka sasa. Naamini nitakuwa mtu mwenye furaha sana nitakapokuwa nakuchukua picha. Maana mimi ndiye mchukuaji picha katika kundi letu hili."

"Nitafurahi sana kuzidi kuonana na nyinyi kwani mnaonekana kuwa watu waungwana sana. je, mnatoka wapi?" Aliuliza.

"Siye tunatoka mjini Mwanza, Tanzania," alijibu Sammy. Kisha Lulu alituaga akaondoka kwenda kucheza dansi. Mimi huwa siwaamini wasichana wazuri kama hawa. Nakumbuka siku moja mama yangu, Mama-Willy, alinieleza kuwa kati ya wanawake wote, ukiona mwanamke mzuri sana jua mwanamke kama huyo ni hatari sana. Na nilipoanza kazi kila siku ninapotumwa kwenye shughuli fulani jambo la kwanza la Chifu ni kunisihi nisifuate wanawake wazuri sana. Maana wanawake kama hao ni sumu kali sana. Lakini mimi Willy, ingawaje nakubaliana na Mama Willy pamoja na Chifu, nimekuja kutambua kutokana na kazi zangu kuwa, kutokana na mwanamke mzuri sana unaweza kupata habari za ajabu sana. Nilikata shauri kuwa sitamwachia Lulu vivi hivi lazima nitafute mengi ya maisha yake.

Huyo mtoto Lulu ni Lulu kweli kweli. Kwani toka kwenye dole gumba mpaka utosini hana dosari yoyote. Ukimwona hutaamini kuwa alizaliwa na mwanadamu ila labda mtoto wa jini, kama unaamini kuwa kuna majini, ama amefyatuliwa kutoka katika mashine baada ya kuchongwa na mchongaji nambari moja hapa ulimwenguni. Nakwambia kama Lulu ataacha wazi sehemu ya kifua chake halafu umtazame, utababaika. Hutaweza kumwangalia mwanamke mwingine yeyote. Utawahesabu wanawake wengine kama wanaume tu. Kama Mungu amewahi kupendelea, basi huyu Lulu amempendelea hasa.

"Sammy," niliita, "angalia kila mtu anayehusiana na Lulu katika hii klabu. Nawe Robin pata watu wa kumfuatia Lulu ili tupate kujua anakaa wapi." Nilinyamaza kidogo kisha nikaendelea, "Mimi itanibidi niende kule hotelini kwa Fred nikajue kuna nini, maana mpaka sasa yapata saa nne na nusu na bado hajaonekana. Ninawaacheni wote hapa ili kuangalia mambo ya hapa klabu. Lakini Sammy unipigie simu kama ukiona nimechukua muda mrefu, zaidi ya dakika arobaini na tano. Na upige kule kule chumbani kwa John. Kwaherini." Nikaondoka.

Nilikodisha gari nje na kwenda moja kwa moja mpaka Ambassador Hoteli. Sikutaka anitelemshe hapo Princess Hoteli. Niliposhuka hapo, ilinibidi nichukue Government Road nionekane kama kwamba nataka kuchukua 'bus' kwenye kituo cha 'mabus' cha Ambassador. Nilikwenda nikazungukia mtaa wa Duke, halafu nikaingia katika mtaa wa Tom Mboya.

Nilipoingia Princess nikakuta watu wengi sana katika baa. Nikajifanya kama miye pia mpangaji wa hapo lakini nilitazama huku na huko hapo hotelini ili nione kama kuna mtu ananichunguza. Lakini watu wote walionekana wakishughulika na unywaji wa pombe na kadhalika. Nilipanda ngazi mpaka ghorofa ya kwanza, Robin alikuwa amenipa nambari za chumba ambamo John alikuwa akilala. Nilikwenda mpaka kwenye hicho chumba. Kabla sijagonga nilikagua vyumba viwili vilivyokuwa upande wa kuume na kushoto wa hicho chumba. Lakini sikuona wa kusikia chochote. Ilionekana hivyo vyumba havikuwa na watu, au wote walikuwa wamekwenda kutembea.

Niligonga kwenye mlango wa John lakini sikusikia lolote. Nikafikiria kutoka, lakini nikaona afadhali niingie ndani pengine nitaweza kupata habari zozote. Ama huenda akawa ameacha habari fulani fulani. Nilichukua funguo zangu malaya ili nifungue mlango kwani ulikuwa umefungwa.

Nakwambia sijawahi kushituka kama nilivyoshitushwa na hali niliyoikuta humo chumbani nilipowasha taa. Hofu iliniingia, nikaanza kugwaya. John alikuwa amelala kifudifudi. Amekufa! Fahamu zilinitoka kwa muda wa dakika tano hivi. Baada ya kuzinduka nikaenda karibu na maiti ya John ili niichunguze vizuri. Niliona kuwa alikuwa amepigwa risasi sita, zote kifuani.

Ilionekana kuwa huyo aliyempiga hizo risasi, bastola yake ilikuwa .45. Kwani miye nimewahi kuona matundu ya risasi hizi. Haya mauaji yalikuwa ya kutisha sana. Yalikuwa mauaji ya kikatili sana, maana aliyemwua alimwachia risasi nyingi kana kwamba alimwua ng'ombe. Na ilionekana kwamba waliingia kwa ghafla, kiasi ambacho hata John hakuweza kujitetea.

Kifo hicho cha John kiliniuma sana hata nikaapa kuwa huyo aliyemwua, lazima nimkamate na kumwua mimi mwenyewe, kama nitakuwa mzima wakati wote wa madhila kama hayo. Woga ulianza kuniingia kwa mara ya kwanza.Tangu nianze kazi hii sijapatwa na woga kama huo. Kitu kilichofanya nitishike sana ni jinsi wauaji hao walivyomfahamu John. Na kama ni hivyo, basi hata sisi tutakuwa tumeisha fahamika. Na kama wameweza kumwua John ambaye ni mpelelezi mashuhuri katika Afrika ya Mashariki, lazima watu hawa wawe miamba kweli. Na lazima wawe ni wenye akili nyingi sana juu ya kuwinda watu.

Kweli tulikuwa tunanuka vifo siye sote. Hazijapita hata saa ishirini na nne, watu watano tayari wameishakufa! Hata kama ungekuwa na moyo mgumu kama wa Farao, hata wewe ungeweza kutishika.

Nilikata shauri, kuufunga mlango na kuiacha hiyo maiti halafu niende kuwapigia simu polisi. Lakini kabla sijatoka niliona heri nipekuepekue mifuko ya John ili huenda nikapata kitu chochote kilichofanya hata wamfuate. Na kama unafikiri sana unaweza kuona kuwa lazima John, wakati sisi tunashangaashangaa yeye alikuwa amegundua jambo fulani ambalo ndilo lililosababisha kifo chake. Kisha nilienda mpaka kitandani ambako kulikuwa na mkoba. Nilipoinama tu,nikasiki sauti ikiniambia,"Tafadhali kaa ulivyo wala usisogee hata inchi moja. La sivyo utapata idadi ya risasi zile zile zilizomwingia huyo mshenzi karibu nawe hapo." 
Nikaduwaa....!

ITAENDELEA 0784296253

Comments

  1. Mkuu,utatuua haki ya nani. Mwezi hadi mwezi? Unajua mkuu Nyakasageni tunakuwa tusha sahau matukio ya last session? Ipige kama ya Alimasi

    ReplyDelete

Post a Comment

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU