KUFA NA KUPONA

SURA YA NNE

Mrembo Lina

Nilipotazama saa yangu, ilikuwa saa tisa na nusu. Nilitoka hapo baa na kukodisha gari hadi Starlight. Niliwakuta Robin na Sammy wakitungojea.

 Robin hakuonekana mwenye furaha. Nadhani Sammy alikuwa amemweleza mambo yalivyokuwa. Halafu niliamua kupiga simu polisi ili waweze kushughulika na hizi maiti. 

"Hapo ni Polisi?".

"Ndiyo Bwana, unataka nini?".

"Naweza kuzungumza na Polisi Inspekta Tsumah?. Tafadhali".

"Ngoja kidogo" alijibu.

"Hallo, huyu ni Polisi Inspekta Tsumah. Nani mwenzangu, na nikusaidie nini?"

"Mimi ni rafiki yako, ambaye ninazo habari za kukugutusha kidogo. Ni kwamba ziko maiti tatu katika Princess Hoteli chumba nambari 51. Nenda ukajionee mwenyewe. Miye sina uhusiano nazo. Kwa heri." nilikata simu kabla hajaweza kusema neno lolote.

Nilipiga simu kwa Chifu saa hiyo hiyo, nikimweleza kuwa awashauri maafisa wa polisi wasishugulike sana na mauaji yoyote yatakayotokea hapa Nairobi mpaka tutakapokuwa tumemaliza kazi yetu. Pia nilimweleza kuuawa kwa John.

Robini alitoa taarifa aliyokuwa amepewa na vijana wake juu ya Lulu. Alisema, "Baada ya wewe kutoka, Lulu naye alitoka. Mmoja wa vijana wangu alimfuata, na ilionekana Lulu alikwenda moja kwa moja hadi International Cassino. Alivyofika huko alisimama nje kwanza. Kisha alitoka kijana mmoja katika International Cassino na kuja kuonana naye. Alinyamaza alipokuwa akimeza mate.

"Walikaa hapo nje kwa muda. Kisha huyo kijana alimpa busu Lulu. Ilionekana kuwa Lulu alikuwa akimtegemea huyo kijana huko Starlight, lakini kijana huyo hakuonekana. Ilionyesha kuwa Lulu alijua kwamba huyo kijana mara nyingi alikuwa akienda Cassino. Alipofika hapo nje kumbe huyo kijana naye alikuwa akitoka. Kijana wangu alifikilia kuwa lazima wawe marafiki. Kijana huyo alionekana nadhifu sana, lakini macho yake yalionyesha uovu mwingi. Kijana wangu hakuweza kusikia waliyokuwa wakisema, ila alibuni kuwa walikuwa wakizungumzia juu ya kitu fulani kuhusiana na Starlight Klabu. 

"Kijana wangu alingoja hapo mpaka walipokuwa wakiondoka. Walipoondoka, Kama alivyoripoti kijana wangu, waliingia katika gari moja Zephyr 6 nambari KKK 117. Walivyoanza safari ya kurudi mjini na Uhuru High Way naye aliwafuata. Walienda na kusimama nje ya Hoteli Intercontinental. Na Lulu alitoka nje. Alipokuwa akiingia hotelini, kijana wangu alimsikia Lulu akimuaga huyo kijana kwa sauti, "Kwa heri Benny."

Kusikia jina la Benny, nywele zangu zilisimama kidogo, kwani yule kijana wa Princess alikuwa pia ameniambia kama unakumbuka. Benny alikuwa amekuja kuchunguza kile chumba nambari 50. Katikati yangu na wewe nadhani Benny ana jambo hapo.

Nami nilimweleza mambo ambayo niliyapata kutoka kwa yule kijana wa hotelini. Nao walianza kumshuku Benny na Lulu pia. Maana kama nilivyosema awali. Kwamba wasichana waliovipande wote ni sumu mbaya sana.

Wote tulifikiria kwa tulikuwa tukianza kuona mwanga kidogo. Lakini hee, makubwa yalikuwa bado yanakuja. kwani kama huyo Benny na Lulu ndiyo wanacheza haya mambo lazima kuna kitu!

Tuliondoka hapo nje ya Klabu na kila mtu akakodisha gari kwenda kulala. Tulikuwa tumepanga, kupigiana simu kesho yake asubuhi mnamo saa mbili. Robin alikuwa akilala New Avanue Hoteli.

Gari niliyokodisha ilinipeleka hadi hoteli Fransae. Kisha niliingia vichocholoni mpaka Embassy Hoteli. Kama mtu alikuwa akinifuata, angeweza kufikili kwamba nilikuwa nikilala hoteli Fransae. Niliingia chumbani kwangu ili nilale. Mawazo yangu yote yalikuwa juu ya mauaji ya John. Niliwaza kumuua huyo aliyemuua John iwapo muuaji huyo hatatangulia kiniua. Kitandani hapo chumbani, niliweka bastola yangu chini ya mto, kwani sikuweza kujua lini watu hao wangenifuata, maana wanaonekana kuwa wajuvi sana. 

Asubuhi niliamshwa na mfagiaji, ambaye alikuwa anafagia nje ya mlango wangu. Kwa bahati mbaya akagonga mlango huo. Nilipotazama saa ilionyesha kuwa ilikuwa yapata saa mbili kasorobo. Nilikwenda kuoga, na kujiweka tayari kwa kazi ya mchana huo. Saa mbili kamili nilikuwa nimekwisha piga simu kwa Sammy na Robin.

Kabla sijapiga simu, Sammy alianza yeye kunipigia akisema, "hallo Willy, vipi? Umelala salama leo? Miye mwenzio nilikuwa na ndoto za ajabu na za kutisha. Nadhani kifo cha John bado kinanitisha. Sasa unasemaje, tuanzeje?"

"Sammy, nadhani haya tusiyazungumze kwenye simu, ila mpigie Robin simu umweleze mje hapa hoteli kwangu. Umeshapata kifungua kinywa ama vipi?"

"Bado sijapata, ila nategemea kupata sasa hivi."

"Vema, tutaonana saa tatu."

"Nililetewa kahawa na kuanza kunywa. Baridi ilikuwa kali sana... Ukungu ulikuwa umejaa kote. Siku ilianza kunitisha sana, hata kabla sijaanza kufanya lolote. Nilionekana mtu mwenye wasiwasi mwingi sana. Ungaliniangalia asubuhi hiyo hata wewe ungalinihurumia, ingawaje mimi si mtu wa kuhurumiwa. Ilipofika saa tatu. Sammy na Robin walifika. Mimi naona twende 'City Hall' maana maonyesho yanaanza leo saa tano. Na kama hamjui, leo ni sikukuu ya kufungua maonyesho. Kwa hiyo watu kote nchini wanapumzika hawaendi kazini. Na kwa sababu Lulu anasema ni mwonyeshaji mavazi, basi lazima atakuwepo. Na kama kweli Benny ni rafiki yake, hata yeye atakuwepo hapo 'City Hall' na kutokana na msongamano huenda tukafahamu lolote," alisema Robin.

'Gazeti la Daily National' lilikuja, na baada ya kuliangalia ilionekana mengi hayakuandikwa juu ya hivyo vifo. Maana waliandika tu ya kuwa "Watu watatu walikutwa wamekufa katika chumba kimoja Princess Hoteli. Polisi bado wanafanya uchunguzi," basi. Tulifikiria mkurugenzi wa usalama Kenya alifanya kama tulivyokuwa tumeomba.

Saa nne na nusu tuliondoka kuelekea City Hall. Sammy alibeba kamera na kuonekana kuwa mpiga picha hasa. Miye nilionekana kama mwandishi wa habari. Tulikuwa tumechukua vitambulisho vyetu. Tulipofika City Hall, baada ya kuonyesha vitambulisho vyetu, tulikuta siye tumepewa viti huko mbele karibu na jukwaa kusudi tuweze kuangalia na kuchukua picha vizuri. Mimi na Sammy tulikaa karibu karibu na Robin alikaa mbali kidogo nasi.

Robin alikuwa ameishafanya mpango na vijana wake kuwa karibu karibu katika huo ukumbi, kusudi ikiwa wataweza kuona lolote waweze kusaidia. 

Kitu kilichokuwa kinaniuma ni kutaka kujua zilipokuwa hizo karatasi za siri. Pia wakati gani wamepanga kuzibadilisha. Na tatu wapi ambako haya mabadilishano yangefanyika. Mpaka hapo tulikuwa tumekwisha hakikisha kuwa Chifu alivyobuni itakuwa sawa. Maana mpaka hapo ilionekana ni watu wa Afrika Mashariki waliotuandama. Kule kujua kwao kwamba siye tumefika Nairobi na kuanza kuwasaka, kungefanya waharakishe kuzibadilisha hizo karatasi, kitu ambacho hatutaki kitokee. unaweza kuona mwenyewe jinsi muda ulivyokuwa mbaya. Akili zetu zilivurugika kama nini sijui.

"Hujambo mwananchi?" Nilisikia sauti kwa nyuma yangu ilinishtua sana kwa maana nilikuwa katika mawazo mengi. Nilipogeuka nikakuta ni mtu ninayemfahamu ambaye alikuwa muda mrefu sana Dar es Salaam. Huyu alikuwa Peter ambaye naye alikuwa mpigania uhuru na sasa akiwa ameletwa Nairobi kufanya kazi.

"Hallo Peter,habari? Mimi ni Joe Masanja nimekuja hapa kama mwandishi wa habari juu ya maonyesho ya mavazi. Na huyu ni Athumani Hassan, Mpiga picha".

Peter alijua nilikuwa na maana gani sababu ananijua, na anajua kazi yangu ni nini.

"Mmefika lini hapa. Lazima liwepo jambo alininong'oneza.

Kisha aliandika habari kwenye karatasi na kunipa. Humo aliandika maneno haya," Jee mmekuja kuchunguza kuhusu tukio la jana? Nimeambiwa na ofisi ya Dar es Salaam nisaidie. Kama ndivyo niko tayari kuwasaidia."

"Tulifika jana. Na hasa," nilijibu.

Peter alielewa, kisha alihama akaja kukaa na sisi. Alikaa upande wangu wa kulia na Sammy upande wa kushoto.

Baadaye nilimuona Lulu anaingia akiwa na Benny. Nilimuuliza Peter, "ati unawajua hawa?"

"Siwajui, ila tu nimewahi kumuona yule Benny katika mabaa fulani fulani tangu nifike hapa Nairobi. Kama ukipenda kujua jambo lolote juu yake hiyo ni kazi rahisi. Ninaweza kukupatia habari kabla ya usiku wa manane leo."

"Nitafurahi sana ukifanya hivyo na watu wako."

Peter alioneka mwenye kuhudhunishwa sana na jambo hili akiwa kama mpigania uhuru. Baadaye Lina naye aliingia. Alikuwa peke yake kama kawaida. "Ulitaka kumuona yule? Nilimuuliza Peter.

Ndiyo. Yeye ni Lina Samson."

Lina alikuwa msichana tofauti sana na wasichana wengine. Sura yake ilikuwa ya kupendeza vya kutosha, kama nilivyosema awali. Lakini licha ya Lina kuwa mzuri wa sifa hivyo, hakufua dafu kwa Lulu, kwani Lulu alikuwa 'Lulu' kweli. Pia Peter alisema utamkuta Lina siku zote peke yake mwenye mabaa akinywa soda akichanganya na 'Babycham'. Hivi ndivyo hata mimi nilimkuta usiku uliopita. Lina alituona akaja moja kwa moja kutusalimia. Kisha akanipigia kope akaenda kukaa mbali nasi kidogo.

Wakati Benny alipoingia na Lulu kila mtu aligeuka kuwaangalia. Lulu alitembea kwa maringo sana na Benny alionekana akifurahia kuona kila mtu akimwangalia wakati wakifuatana na mrembo huyo wa kushtua. Hata mimi nilimuonea wivu. Maana nilitamani niwe mimi badala yake nitembee na mrembo huyo. Lina alimwangalia sana Lulu. Nikaona huenda alikuwa pia akimuonea haya Lulu. 

Nilitambua kuwa Lina anamfahamu Benny, kwani Benny alipokuwa anapita na Lulu, alipomuona Lina amekaa karibu na mahali walipokuwa wakipita, alitazama chini. Kwa hiyo niliona itakuwa vizuri kama nitafanya urafiki na Lina maana naweza kupata msingi mdogo wa kutusaidia. Pia niliona Lina angeweza kusikilizana na mimi, kwani kama nilivyosema alinipigia kope kuonyesha dalili ya urafiki.

Maonyesho yalipoanza wanawake walianza kutoka mmoja mmoja wakionyesha mitindo ya kila aina. Kulikuwa na wanawake kutoka karibu kote Ulimwenguni wakitoa mitindo mbali mbali. Niliandika kikaratasi na kumpa Sammy akiangushe katika mapaja ya Lina, wakati akijifanya kama kwamba anatafuta mahali pazuri kwa kupiga picha. Niliandika, "Tafadhali tuonane nje, kwenye mlango mkubwa, kama dakika kumi kabla ya watu wote kutoka. angalia watu wasifahamu unaningoja mimi************".

Sammy alikiangusha kama nilivyomueleza. Baada ya kusoma bila mtu kujua aliniangalia na kutikisa kichwa, akionyesha kuwa amekubali. naye alianza kuandika kwenye hicho kikaratasi. Akakitupa mbele ya Sammy. Alipokuwa anarudi. Sammy alijifanya ameangusha kasha la 'Film', akainama na kukiokota hicho kikaratasi pamoja na kasha la 'film' yake. Niliposoma nikakuta maneno haya. *************"Ndani ya gari langu jeusi namba No. KKT 581 - Mazda Delux - kulia mwa mlango mkubwa," basi niliona mambo yote yamekuwa kama nilivyopanga. Lakini ukavu wa macho ya Lina ulinitisha kiasi cha kwamba woga uliniingia kidogo. Lakini kwa sababu sikuwa mwoga kama wewe, sikujali lolote litalotokea baadae.

Lulu alijitokeza. Alipotokea kwenye jukwaa kila mtu alipiga kelele, kwa vifijo na ushangiliaji wa ajabu. Lulu aling'aa kama nyota. Alionyesha mtindo wake unaoitwa 'Popcom'. Wachukuaji wa picha walichua picha kwa fujo sana.

Alipokuwa anarudi kwenye chumba wanachotokea. Robin alipita karibu yangu na kudondosha kikarasi. Nikakisoma kilikuwa kimeandikwa "Mjiangalie sana, maana yametokea mauaji mawili tayari humu ndani", wakati Lulu alipotoka na watu walipokuwa wakipiga kelele na kushangilia vibaya sana, vijana wetu tuliokuwa tumewaweka kuviziavizia, wawili wao wameuawa. Inaonekana waliona jambo fulani ambalo limewaponza. Mueleze na Athumani, laa zivyo na siye tutakufa".

Lo wasiwasi ulinizidi sana. Sammy alipokuja karibu yangu nilimueleza mambo yalivyokuwa. Zilikuwa zimebaki kama dakika kumi na tano hivi maonyesho ya asubuhi yaishe. Hivyo tukafungashafungasha vijitabu vyetu tuondoke. Tulimuaga Peter baada ya kumweleza ninapokaa. Tulitazama huku na huku kwa mashaka makubwa sana. Nadhani hata wewe unaweza kufikiria mawazo tuliyokuwa nayo.

Tulipofika mlangoni, nilibahatisha kumuona Benny amesimama na kijana fulani akimueleza mambo fulani fulani na huku akitutizama kwa usiri mno. Nilijua alikuwa akimuambia huyo kijana atufuate. Hivyo nilimueleza Sammy abaki nyuma kidogo ili niweze kuwapoteza wasije wakajua ninaondoka na Lina.

Peter alikuwa kwenye dirisha moja la 'Hall" na akaniona nilipokuwa nikiingia katika gari la Lina. Akanipungia mkono. Nadhani aliweza kupata nafasi ya kukisoma kikaratasi cha Lina. Sikujali Peter kufahamu hayo, kwani na yeye ni mtu wetu.

"Mtu yoyote amekuona?"

"Hapana, uenda wamekuona wewe" alijibu.

"Sidhani kama wameniona"

Lina alitia moto tukaondoka. "Tupitie njia ipi?" aliuliza.

"Twende moja kwa moja, mpaka Embassy Hoteli." 

Lina alivuta gari mpaka tukaingia Kenyatta Avenue. Nilipotazama nyuma, niliona gari moja kama kwamba linatufuata. Kutaka kuhakikisha nilimueleza Lina badala ya kuingia Koinange akate kona na kuingia uhuru High Way. Halafu aingie Haile Selassie Road. Gavament Road ndipo turudi Kenyatta Avenue. Kisha tuendelee na safari yetu. Kusema hili gari lilikuwa linatufuata maana kuzunguka kote huku nalo lilikuwa bado linazunguka kutufuata tu. Tulipofika kwenye kona ya Kenyatta Avenue nilimwambia Lina asimame, aliposimama hilo gari nalo likasimama karibu sana nasi. Nilitoka nje nikamfuata dereva wa gari hilo. 
"Sikiliza bwana mdogo, Miye sitaki kufuatwafuatwa. Sikuzoea mambo hayo. Na kama hutaki meno yako zidi kunifuata. Kamwambie huyo mume wako aliyekutuma kuwa kama anataka kunitafuta aje yeye mwenyewe ajionee. Kama unataka usalama tia gari lako moto uende zako."

Kijana huyo hakuwa na la kufanya ila kufanya kama nilivyomwambia. akaenda zake. Nilirudi katika gari la Lina akaendesha mpaka Embassy Hoteli. 

"Sikiliza Lina, nenda ukasimamishe gari hili mbali na Embassy Hoteli kusudi hawa wahaini wasijue tuko hapa wakatufuata"

Baada ya kuweka gari Lina alikuja tukapanda mpaka kwenye chumba changu. "Sijui kwa nini naonekana kukupenda, maana tangu jana mle Princess Hoteli, baada ya kutoka na kukuacha humo, usiku mzima sikulala ila kukufikiria wewe tu." Alisema Lina hali akijilaza. 

"Oh Joe, mpenzi nakupenda sana ingawaje unaweza kuniona kuwa miye malaya kwa kukufuata baada ya kuonana siku moja tu. Lakini lazima ujue kuwa mtu unaweza kuwa hujapenda, lakini akaja mtu mgeni ukampenda kufa. Hapa Nairobi nimeishawahi kufanya mapenzi na mtu mmoja tu, ambaye anaitwa Benny Makunda. Lakini hata siku moja sikuweza kukosa usingizi juu yake, kama nilivyokosa juu yako jana. Ningejua unakaa hapa basi tu ningekufuata."

"Waaa, unasema kweli ama tu kunidhihaki? Hata mimi nimekupenda Lina. Tangu jana tabia yako ya utulivu na kiburiburi niliipenda sana. Maana mimi napenda watu kama hao hasa wakiwa wasichana" 

Loo! Hapa niliona mambo yanakorogana sana Benny aliwahi kuwa mpenzi wa Lina. Na Benny ndiye tuliyekuwa tunamashaka naye. Huyu kijana anaonekana ni 'Champion' kwa wanawake, kwani sasa anatembea na Lulu. "Huyu msichana Lina ananitania ama vipi." ndiyo sasa yalikuwa mawazo yangu. "Lakini yote hayo nitafahamu muda si mrefu kwani naweza kumusoma msichana kama Lina Vizuri sana."

"Kumbe unamfahamu Benny, hata amewahi kuwa mpenzi wako?" Nilimuuliza.

"Ndiyo," alijibu.

"Mmeachana tangu lini?"

"Kuna huyu msichana wanayemwita Lulu. Msichana huyu anatoka Uganda na huwa yuko huku mara nyingi sana. Sura yake kama ulivyomuona inavutia wavulana wengi sana. Alipokuja huku mwezi wa jana Benny alimuona, na wakaanza mapenzi. Mwishowe Benny hakunijali tena. Nami kwa tabia yangu nikaona siwezi kupenda mtu ambaye hapendeki.

"Kwanza nilimuonya Benny asitembee na Lulu kwani Lulu ingawaje ni mzuri kiasi cha kutisha namna ile, lakini ni hatari sana kwa mambo ya ukahaba. Lakini baada ya muda mfupi Lulu alirejea Uganda. Benny akarudi sasa. Lakini miye sikumtaka tena.

"Benny ana fedha na ana fedha nyingi. anazitoa wapi sijui, lakini ana fedha. Kazi yake ni dereva wa taksi tu. Anaendesha taksi yake moja 'Mercedes Benz'. Nilipokataa Benny alinibembeleza sana lakini nikakataa tu bado. Aliniahidi kuwa angelininunulia gari moja aina ya 'Citron' mwezi huu, maana atakuwa 'Giriki' mwezi huu. Miye nilizidi kukataa tu. Na nilikuwa nimeapa hata siku moja sitafanya mapenzi na mvulana tena. Nilikuwa nafikiria kwenda kuwa mtawa. Bahati nzuri au mbaya ndipo akaja huyu kijana ambaye amenifanya hata sikuweza kulala. Oh, kweli mama aliniambia usimpende mgeni, lakini mimi hata, nitakupenda tu."alimalizia Lina.

Bado mimi sikumwamini hata punje.

"Benny alikwambia hiyo pesa angetoa wapi?" Nilimuuliza.

Alisema ati ana rafiki zake huko  ng'ambo ambao wangemletea fedha hiyo. Benny anafahamiana na wazungu wengi sana," alisema kwa mashaka kidogo.

Ubaya wa huyu msichana ni kuwa huwezi kumwelewa hata kidogo kwani anaposema, husema kwa utulivu mno hivyo kwamba huwezi kumtambua yupo upande upi.

"Unaweza kuwatambua wazungu hawa ukiwaona?"

"La, wengi wao wamerudi kwao. Ndiyo sababu nakueleza kuwa, watamtumia pesa kutoka ng'ambo waliko," alijibu.

"Unafikiria ni Wazungu kutoka upande gani?"

"Sijui maana mimi nilikuwa sihusiani nao sana."

"Ni wanaume au wanawake?" Nilimwuliza huku nikijifanya siyajali sana mazungumzo yake haya.

"Lo, Joe, mimi sikuja hapa kujibu maswali juu ya Benny. Mimi nimekuja kwa sababu napenda kuzungumza juu ya maisha yangu na wewe na kufanya mapenzi. Kama unatafuta wanawake wa Kizungu, ambao Benny hutembea nao, ni rahisi sana kuwapata hapa Nairobi. Na kwa vile wengi wamekuja kwenye maonyesho, nenda tu ujipige utapata," alijibu kwa uchungu sana na hasira.

"Si hivyo Lina. Sina haja na wanawake wa kizungu, ila tu nilitaka kufahamu mengi juu ya Benny, kwani anaonekana anawakosha sana wasichana. Mtu wa kuweza kumuacha msichana wa haiba kama wewe, lazima awe mwamba hasa."

"Lakini unanipenda kweli Joe?" Alisema huku machozi yakimtoka.

"Ninakupenda sana Lina. Na sasa ninaanza kukuelewa na kukupenda zaidi. Je. Benny anakaa wapi?"

"Benny anakaa huko Westlands, karibu na maduka ya Westlands. Nyumba "plot No. 3" pembeni mwa Nakuru Road, baada ya kuvuka Motel Agip. Au kwa urahisi karibu na Sclaters Hostel."

"Mpenzi Lina, nataka kukuambia ukweli sasa. Mimi si Joe Masanja, mimi ni Willy, Willy Gamba." Lina alikuwa amelala kwenye kitanda lakini nilipotaja hilo jina, aliruka na kusimama mbele yangu huku anaonyesha hali ya kushangaa sana. 

"Mimi ni mpelelezi wa Idara ya Uchunguzi ya Tanzania." Nilitoa kitambulisho changu cha upelelezi. "Usishtuke Lina, Kaa chini na huenda toka sasa tutaelewana vizuri zaidi. Na huenda toka sasa ukanisaidia." Nilienda kukaa karibu naye hapo kitandani.

Alinivuta akaanza kufungua tai yangu, kisha shati langu, halafu suruali yangu... tukajilaza.

ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU