KUFA NA KUPONA

SURA YA TANO

"Hatari City Hall" 

"Wuuuuu. Willy, Willy Gamba, umesema ndiye wewe! Loo! Siamini masikio yangu ni wewe kweli, kweli! Nimesikia jina lako mara nyingi. Nimesikia sifa zako. Nilikuwa nikidhani ni hadithi tu kama tunazosoma katika vitabu. Sikufikiria ama kuota kama nitakuona. Nimesoma habari zako katika magazeti, lakini nilikuwa sijaota ya kuwa siku moja nitalala kitandani na Willy Gamba." alisema Lina huku akitetemeka na kunibusu, "Nini kimekuleta sasa hapa, Willy?" aliuliza.

Nilifikiria sana kama naweza kumwambia. Mwishowe nikakata shauri nimwambie kwani siye nyakati zingine huwa tunaropoka kusudi tuone nini kitatokea. Mara nyingi huwa tunajitega wenyewe halafu tunatafuta njia ya kujinasua tena. Hivyo nilimweleza mambo yote tangu mwanzo mpaka mwisho. Pia nilimweleza jinsi tunavyomfikiria Benny. Na jinsi ambavyo tumenusurikanusurika usiku wa jana. 

"Jana usiku nilipokuwa nikitoka nilimuona Benny hapo nje ya Princess katika gari moja ya Kimarekani 'Pontiac' yeye hakuniona" aliniambia Lina.

Kama Lina anasema kweli basi Benny ndiye alipanga mauaji ya John na kama nilivyokwambia ahadi chuki na uchungu viliniingia juu ya Benny.

"Je unamjua rafiki yake yeyote wa Kireno au wa Afrika ya Kusini?" 

"Hapana lakini naweza kukusaidia ukitaka," alijibu.

"Kukuambia ukweli Benny si mchezo. Anatembea na bastola tatu, na kila nilipokuwa nikimuuliza ni za nini aliniambia kuwa ni za kujikinga kutokana na maharamia. Maana akiwa na taksi, wanaweza kuikodisha halafu kufika njiani wakakunyang'anya, hasa mtu mwenye 'Benzi' kama yeye. Tena akipiga risasi zake hazikosi. Maana siku moja tulikwenda msituni kuwinda katika bonde la ufa, ndipo nilimtambua. 

"Tulikuwa na mdogo wake ambaye alibeba chupa za fanta ndogo. Basi alikuwa anaweka hizo chupa kwenye kichwa cha mdogo wake na kuanza kupima shabaha kwa bastola. Ajabu ni kwamba hakuweza kumjeruhi mdogo wake hata kidogo. Na aliniambia kuwa huwa anafanya haya mazoezi mara mbili kwa juma. Hivyo nakusihi Willy usimuendee ovyo. 

"Asante sana kwa kunionya Lina maana kama ningalikurupuka huenda hata mimi ningeyala marisasi kama rafiki yangu John."

Mara simu ililia. "Huyu ni Peter nazungumza, ni Joe huyo?"

"Ndiyo Peter unataka nikupe hadithi gani?"

"Sikiliza Joe, nina habari. Nimepata habari kamili juu ya maisha ya Benny, Benny anakaa Westland 'plot No. 3' karibu na Sclatirs Hostel. Yeye ni dereva wa taksi. Anaendesha taksi moja aina ya 'Mercedes benzi 280 SE'. Nambari KKZ 601. Rangi ya kijani. Benny anafahamika kuwa kijana tajiri sana, maana hilo gari lake linapendwa na watu wengi hasa watalii. Hivyo anafahamiana na watalii wengi sana. Amesoma mpaka darasa la kumi na nne. Kisha akaenda nchi za ulaya, ambako inasemekana hakufanya vizuri katika mtihani wake ikapasa arejee. Amewahi kukaa ureno kwa muda fulani fulani huko. Ni kijana fundi sana katika kutumia bastola. Ana shabaha za ajabu. Walimuomba aende jeshini akakataa. Polisi huwa wana mashaka naye kuwa uenda akawa naye ndiye mmoja wa magaidi wa hapa Nairobi wanaonyang'anya mali katika maduka makubwa makubwa na benki. Lakini hawajawahi kumshika ila wanamfikiria tu. hajapelekwa kontini hata siku moja. Tabia yake ni ya utulivu sana, lakini ni shupavu sana na mvumilivu wakati wa shida. Wasichana wengi sana wanakufa kwake kwa sababu ana sura nzuri. Kama onavyomuona. kwa kifupi ndivyo mambo yalivyo."

"Asante Peter, endelea kufanya uchunguzi uwao wote ambao unaweza kutusaidia." 

"Miye nitajaribu kila njia ya kuwasaidia. Na kama una shida nyingine yeyote unaweza kunieleza tu. Kwa kheri mpaka wakati mwingine."

Nadhani hata kama huwa unatumia makamasi badala ya ubongo, unaweza kuona mambo yanavyokuja yenyewe. Benny anafahamu kutumia bastola vizuri sana. Kwa hiyo Benny analo kundi la watu ambao amewafundisha namna ya kutumia bastola nao wamekuwa stadi kama yeye. Benny amekaa ureno kwa muda, na alipokuwa huko alifanya urafiki na watu wa huko na hata akaweza kutumia bastola vizuri sana. Ni wazi kuwa hao wareno wamejua habari za hizo karatasi za siri. Wakakata shauri waziibe.

Wamejaribu wao wenyewe na kushindwa. Waliposhindwa na kuona wao hawawezi kuziiba wakatafuta majambazi wa hapa hapa Afrika ya Mashariki. Kwa sababu wanamjua Benny na amewahi kuwa rafiki yao wakamwendea. Walipomwendea Benny akaona hawezi maana hana fedha ya kutosha. Lakini Benny anajua kundi fulani la majambazi, kwa hiyo akaenda kumwambia 'bosi' wa hayo majambazi juu ya wizi wa karatasi hizo. Na, pia kuahidiwa kupata fedha nyingi sana. Huyo 'bosi' akakubali. 

"Kisha akamfanya Benny mkubwa wa genge hilo akapewa pesa, gari na kila kitu. Sasa shida ikawa watazipataje, kwa hivyo wakatafuta mtu mwenye kujua habari nyingi juu ya hizo karatasi na kuwapa mambo yote. 

"Umeona basi mambo yalivyo? Kufika hapa sasa naanza kuona mwanga. Ila kuna maswali ya kujiuliza. Je huyu bosi ni nani? Je nani aliye na karatasi sasa? Tutawashikaje maana wameisha tufahamu. Huyu aliyetoa habari ni nani? Na wakati gani hivi vitabadilishwa? Na nani aliyekuja kuzichukua hizo karatasi toka Ureno?.

Ukinijibu maswali haya, nadhani tutakuwa tumemaliza kazi yetu. Lakini rafiki yangu, inaonekana kabla hatujajibu maswali haya tunaweza kuwa wote tumeisha kufa, maana kuyajibu, kuna maana ya ua au uuawe. Ureno, hii ni kazi ya Ureno. Kwa hiyo lazima mwenye kuzichukua kuzipeleka Ureno ni mwenye asili ya Kirenoreno. Na kama kubashiri kwangu ni sawa naona tunaweza kufanya kitu , lakini kama ndiyo nimekosea, basi tumekwisha kazi kabisa."

"Lina," nilimwita hatimaye, "tafadhali jaribu kuchunguza lini Benny alianza kuwa dereva wa teksi. Pili lini amenza kukaa huko Westlands, maana najua ni watu wenye fedha sana tu wanaoweza kukaa huko. Tatu, kama unaweza, jaribu kupata habari za Wazungu anaotembea nao Benny siku hizi. Ukiwa kama msichana wake wa zamani, ukijifanya bado unampenda, kwa hiyo unajaribu mrudiane, nadhani unaweza kupata majibu ya maswali yangu. Pia jaribu kuchunguza ni Wazungu wa kutoka wapi hao rafiki zake." 

Niliagana na Lina akaenda zake. Nilijilazimisha kumwamini. Na kama nilikuwa nacheza na moto, Mungu ndiye anayejua. Kwani Chifu alisema, "Mara hii usiamini mwanamke yeyote."

Mnamo saa nane Sammy alikuja chumbani kwangu. Akanieleza, "Unajua Willy, huyu msichana Lulu pia ni hatari. Maana kila alipokuwa akitoka kuonyesha mavazi anafanya maringo kiasi cha ajabu hata watu wote kushangilia. Na wakati wanaposhangilia ndipo watu wanauawa.

Kwa hiyo inaonekana kuwa kila Lulu akitoka hawa watu huwa wameona hatari kwa upande wao hivyo hupeana ishara. Lulu anatoka, watu wanashangilia, wao wanaua!" 

"Sasa wewe unafikiria tutaendelea vipi?" Nilimuuliza baada ya kumweleza yote niliyokuwa nimeambiwa na Lina pamoja na Peter.

"Mimi naona kuwa twende kwenye maonyesho ya saa kumi. Na twende tukitahadhali sana. Kitu tutakachotafuta ni mtu anayeruhusu hao wanawake kutoka. Tukimfahamu huyo basi tunaweza kujua mengi. Na pia lazima tumpate Lulu tuweze kujua anajua kiasi gani cha habari hii".

Nilikubaliana na mawazo ya Sammy, kwa hiyo tulimpigia Robin Simu kumweleza jinsi tulivyokwishakata shauri la kwenda maonyesho ya saa kumi. Naye alituambia kuwa angekuja kutupitia hapo chumbani kwangu. Mpaka sasa tulikuwa tumejua kuwa wameishatufahamu, la sivyo wasingelinifuata wakati nilipokuwa nikija nyumbani na Lina.

Robin akaja saa tisa na nusu, tukaanza safari kwenda zetu 'City Hall'. Kila mtu alikuwa amechukua bastola kwapani kama ingekuwa lazima itumike.

Tulienda tukakaa kwenye viti vyetu vil evile vya asubuhi. Peter naye alikuja akakaa karibu yetu tena. Lina hakuonekana mchana huo, watu wengi walikuwa wamekuja huo mchana na ukumbi wote ulijaa.

Kama kawaida ya Benny na Lulu walikuja wamechelewa kidogo. Kila mtu alipiga makofi walipokuwa wakipita. Lulu alivaa 'mini' moja inayoonyesha mapaja yake kwa uwazi mno kabla hajaenda kwenye chumba cha maonyesho, Lulu alimvuta Benny wakaja moja kwa moja mpaka tulipokuwa tumekaa mimi, Sammy na Peter. Benny hakuwa na furaha alipotuona. alionyesha kicheko, lakini kicheko chake kilikuwa cha chukichuki.

"Nadhani hamtajali kama nitawafahamisha kwa rafiki yangu huyu,"alisema Lulu.

"Hatutajali," alijibu Sammy.

"Huyu anaitwa Benny Makunda, dereva wa Teksi na ni rafiki yangu." Kisha aligeuka kwa Benny akasema, "Na huyu ni Joe Masanja, yule ni Athumani Hassani, wote waswahili kutoka Mwanza wamekuja kwenye maonyesho ya mavazi hapa petu, maana wao ni waandishi wa habari."

"Nimefurahi kuonana nanyi. Bila shaka mnaipenda hali ya hapa petu Nairobi," alisema Benny, huku tukishikana mikono.

"Nasi pia tumefurahi sana kukutana nawe. Na hali ya hapa inaonekana kuwa baridi, lakini tunaipenda, "nilijibu kwa niaba ya wenzangu.

"Mtakaa hapa muda gani?" aliuliza Benny akinikazia macho.

"Mpaka mwishoni mwa wiki," nilimjibu.

"Na mkitoka hapa mtarudi Mwanza, ama mtaenda mahali pengine?" aliuliza Lulu.

"Tutaenda Kampala," nilimjibu huku nikitabasamu kidogo.

Nakwambia tabasamu la Lulu, ni hatari, maana alipotabasamu nikasisimkwa na damu vibaya sana. Lulu na Benny walitupiana macho kisha wakatuaga, wakaenda zao.

Maonyesho yaliendelea kama kawaida. Nilitoka hapo nilipokuwa nimekaa nikaenda pande za ukutani, ukutani ambako ningeweza kuona vizuri Benny anafanya nini.

Nilimuona Benny akizungumza na Lulu katika chumba kimoja cha kubadilishia mavazi, maana mlango ulikuwa umefunguliwa. Kisha alimwendea kijana mmoja ambaye alikuwa amevaa vizuri sana huku akivuta mtemba. Huyo kijana, kule kumwona tu, utafikiri kuwa ni mwunguna sana.

Walizungumza kwa muda mfupi kidogo, lakini huyo kijana alionekana hapendelei hayo mazungumzo kwani alikuwa na wasiwasi sana. Baadaye nilikuja kutambua kuwa ndiye mruhusuiji wa wanawake kutoka katika chumba cha kubadilishia mavazi kwenda kwenye jukwaa. Wanawake walikuwa mara kwa mara wakitoka na kuingia.

Mwishowe nilimwona Benny akiirekebisha tai yake kwa kuivuta vuta, baada ya kijana furani kupita karibu naye na kumpa kijitabu. wakati huo wote huyo kijana alikuwa akiendesha mpango wa jukwaani alikuwa akimwangalia Benny kila baada ya nusu dakika. Hatimaye kijana huyo alikimbia moja kwa moja hadi kwenye chumba cha kubadilishia mavazi na kuzungumza na Lulu. Ilionekana ilikuwa zamu ya msichana mwingine kutoka lakini huyo kijana alibadilisha mpango na kumfanya Lulu atoke muda huo.

Moyoni nilijua kuna jambo, kutokana na tulivyoelewa asubuhi. Nilijiweka tayari, maana ilionekana huenda mimi ndiye nimetiliwa mashaka. Kwani wanaweza kuwa wameniona nikichunguza mienendo ya Benny, alipokuwa akizungumza na kijana wa kwenye jukwaa pamoja na Lulu.

Lulu alipotoka alikuwa amevalia Mufti. Mara hii alikuwa ameonyesha mtindo mwingine unaoitwa 'love at night' yaani 'mapenzi wakati wa usiku'. Kweli ulitisha kwani mwili wa ndani wa Lulu ulikuwa ukionekana kabisa. Kitambaa cha vazi hilo kilikuwa kama kioo. Ungeweza kuona ndani bila taabu hata kidogo. Umati mzima ulipiga kelele, na watu hawakuweza kuinua macho yao, maana kama unataka kujipatia taabu wewe mwangalie huyo mtoto kwenye jukwaa.

Kwa sababu mimi nilikuwa na mashaka sikuwa kipofu. Niliangaza huko na huko. Ghafla nikasikia mtu anaanguka nyuma yangu huku ameshikilia bastola karibu kufyatua. Watu hawakutambua maana kila mtu macho yake yalikuwa kwenye jukwaa. Nilipoangalia nyuma niliona mtu huyo amekufa kwa kupigwa risasi. Kabla sijakimbia toka hapo, na bado Lulu anavutia watu kwenye jukwaa. Sammy alipita na kuniangushia kijikaratasi. Niliangaza nione Benny alipo sikumwona. Kwa hiyo niliharakisha kutoka kwenye maiti hiyo na kukimbia hadi nilipoketi awali kabla ya mtu yeyote kunitambua.

Lulu alichukua muda mrefu kwenye jukwaa, hivyo alinipa muda wa kuweza kurudi na kukaa bila mtu kutambua. Kwani wakati huo Lulu bado anawapa watu wote moto kiasi cha kutojitambua.

Nilikaa na kusoma kikaratasi hicho. Utashangaa nikikueleza. Mtu huyo aliyepigwa risasi nyuma yangu nilidhani ni mmoja wa vijana wa Robin kumbe hapana. Huyo mtu alikuwa anakuja kuniua mimi. Maana walikuwa tayari wametambua kwamba nitakuwa nikichunguza mienendo ya Benny. Kwa hivyo walimkonyeza Benny. Naye Benny akapanga namna ya kuweza kunitupilia mbali. Mtindo wao waliotumia ni ule ule. Benny anampa ishara yule kijana wa kwenye jukwaa alafu kijana huyo anamtoa Lulu nje. Kisha Lulu anapofika kwenye jukwaa, anatia watu wote moto kiasi cha kutojitambua. Ndipo watu wa Benny wanapopata muda wa kuua mtu wao wanayemtaka bila kutambuliwa wakitumia bastola iliyo na kiwambo cha kuzima mlio.

Mpango huo huo ndiyo uliotumika kwa kutaka kuniua. Lakini bahati nzuri Sammy alishikwa na mashaka. Wakati Lulu alipotokeza aliniona mimi nimekaa mahali wanapoweza kunidhulu vizuri sana. Kwa hiyo yeye aliweka macho yake yote kwangu. Kumbe alikuwa sawa. Jamaa mmoja alitokea kwenye mlango mmoja unaotokea chooni ili aje animalizie mbali. Basi alikuja taratibu. Alipofika karibu alitoa bastola ili kufyatua. Kumbe Sammy naye alikuwa ameishamtilia mashaka akamuwahi kabla ajafyatua. Alikufa papo hapo bila mtu yeyote kutambua na Sammy akapita mahala pangu na kunitupia hicho kikaratasi bila kutambulikana. Kisha tukaenda mahali petu bila kutambuliwa.

 Benny aliingia kutoka nje wakati Lulu alipokuwa akitoka kwenye jukwaa akirudi kwenye chumba cha kubadilishia mavazi. Benny aliponiona alishtuka sana. Rangi yake ikambadilika. Nywele zikasimama na jasho likamtoka. Akaenda moja kwa moja upande wa chooni. Nilimwangalia kwa usili sana alipoiona hiyo maiti ya mtu wake, akajiuma vidole na kwenda zake kwenye kundi, ndipo watu wakaigundua maiti hiyo. 

Polisi waliitwa mara moja kila mtu akaanza kuulizwa ulizwa. Mapolisi walianza kukagua waone iwapo alikuwapo mtu mwenye bastola. Siye tulifahamu kuwa jambo linaweza kutokea hivyo bastola zetu tulikuwa tumeshampa mmoja wa vijana wa Robin na alikuwa ametoroka nazo tayari.

Huyo kijana wa kwenye jukwaa alipoulizwa na polisi kama alimuona mtu upande huo, mara moja alinitaja mimi. Polisi walinijia kuniuliza.

"Wewe ni nani?"

"Mimi ni Joe Masanja, mwandishi wa habari za maonyesho ya mavazi toka Mwanza,"nilijibu.

"Kwa nini ulikuwa umesimama upande ule wakati maonyesho ya mavazi yakiendelea, na hali watu wengine wote walikuwa upande huu?" 

"Mimi kama mwandishi wa habari, niko huru kusimama mahali popote ninapoona ni pazuri kuwezesha kutazama mambo yote na kuandika kwa ufasaha." Nilimwambia huku nikionyesha hasira kidogo.

"Je ulimuona mtu yeyote akipigwa risasi karibu na wewe?"

"Hapana."

"Je, maiti hiyo ilikuwepo wakati ulipoenda kusimama pale?"

"Hapana."

Walianza kunikagua na wakanikuta bila ya silaha yoyote. Yule kijana wa kwenye jukwaa alikuja akaulizwa kama aliniona nikiwa na mtu yeyote hapo pembeni, akasema hakuona. 

"Je, ulirudi wakati gani mahali pako, yaani hapa ulipo sasa?" waliendelea kuuliza.

"Nilirudi baada ya kuandika mambo yangu ambayo nilikuwa nahitaji."

"Kama dakika ngapi hivi zilizopita?"

"Sikutazama saa lakini ni wakati huyo msichana aliyeonyesha mtindo 'Love at night' alipokuwa akiingia tu kwenye jukwaa."

Waliniacha wakaendelea na kuhoji watu wengine. Sammy alikuwa ameniponyesha tena, la sivyo ningalienda kumsalimia babu yangu huko ndani ya udongo. 

Maonyesho yalifungwa mpaka kesho yake saa kumi. Hii niliona itatupa muda wa kufanya kazi kama wakichaa. Na niliapa lazima nimpate Benny na vikalagosi vyake kabla hajafaulu kunitupilia mbali. Maana mara mbili sasa ninaponea chupuchupu.

Watu walipokuwa wakitoka mimi nilikuwa nikimvizia huyo kijana wa kwenye jukwaa. Alipotoka tu nikamfuata. Huku nikimuacha Sammy na Robin waendelee na uchunguzi mwingine. Huyo kijana aliingia kwenye gari na kuanza kuondoka. Alikuwa peke yake humo garini. Mimi nilichukua gari moja niliyokuwa nimefanya mipango na idara ya uchunguzi waniletee. Nilipotoka tu nikakuta  kijana mmoja tayari ameileta hiyo gari. Gari hiyo ilikuwa ya aina ya 'Zephyr 6' ambayo hukimbia sana. Niliweka gari moto nikamfuata huyo kijana. Nilihakikisha kuwa sifuatwi, ila tu Peter ndiye alipita karibu yangu nikampungia mkono. 

Huyo kijana aliendesha gari yake kuelekea pande za Pangani, kwa hiyo nami nilielekeza gari langu huko huko. Niliacha magari matatu hivi mbele yangu kusudi asije akawa na mashaka akiona gari linamfuata katika kila kona aliyokuwa amepita. Lakini nilihakikisha kuwa sitampoteza.

Tulipofika kwenye nyumba za ghorofa za Pangani, huyo kijana alikwenda mpaka kwenye nyumba moja ya ghorofa na kusimamisha gari lake na kutoka nje. Mimi nilihisi kwamba hapo ndipo alipokuwa akikaa. Saa hizo giza lilikuwa limeishaingia hivyo nami nikasimamisha gari langu katika sehemu moja, halafu nikaenda kumvizia huyo kijana. Alipanda mpaka ghorofa ya tatu. Akafungua mlango wa chumba kimoja na kuingia ndani. Wakati huo mimi nilikuwa nimesimama hapo chini nikimwangalia. Kisha na mimi nikapanda mpaka ghorofa ya tatu.

Ghorofa hiyo ilikuwa na vyumba vitatu, yaani jamii tatu zilikuwa zikiishi kwa kila mmoja. Nilipochunguza, niliona kuwa watu katika vyumba vingine hawakuwemo. Watakuja wakati gani, hiyo haikuwa shida yangu wakati huo. Nilichungulia kwenye chumba cha huyo kijana nikamuona akiwa amekaa kwenye sofa hali akivuta sigara. Alionekana bayana kwamba hakuwa na furaha hata kidogo.

Nilibisha kwenye mlango, na nilipokuwa nikifanya hivyo, nilikuwa nikimchungulia kwa dirishani. Kabla hajaja mlangoni akaonekana kubabaika sana hata sigara kumdondoka toka mdomoni. Alijiachia huku na huku kisha akafungua kabati lake la nguo. Akapapasa katika mfuko wa koti moja na kutoa bastola! Ndipo akaja mlangoni kunifungulia huku ameshika bastola hiyo mkononi. Naona hata yeye alikuwa akihisi kuwa lazima lilikuwepo jambo.

ITAENDELEA 0784296253



Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU