KUFA NA KUPONA

SURA YA SABA

Makubwa Tena.

Nilitelemka taratibu kabisa mpaka chini. Hapo chini sikumkuta mtu yeyote, licha ya Sammy niliyetegemea kumuona. Niliingia katika gari yangu mpaka hotelini kwa Sammy. Nilimkuta Sammy akisoma gazeti liitwalo. 'The Detective' nilimweleza mambo yote niliyoyapata kutoka kwa Lulu

Sasa tulianza kuelewa mambo yote yalivyo, "Inaonekana Lulu ameingizwa katika mpango huu kusudi amsaidie Benny katika mambo fulani fulani. Mojawapo likiwa kama yale aliyokuwa akiyafanya maonyeshoni. Laiti isingekuwa sababu kama hiyo basi Benny asingefanya mapenzi na kupoteza fedha nyingi kwa Lulu. Pia tulianza kutambua kuwa Benny siye 'Bosi' ila 'Bosi' mwenyewe yupo', na Benny ndiye msaidizi wake. 

Hivyo zile karatasi anazo 'Boss'. Na anayemjua huyo 'bosi' ni Benny peke yake wengine wanadhani 'Bosi' ni Benny. 

Kwa hiyo kazi kubwa sasa ni kutafuta kwa kila njia tumjue huyo 'bosi' ni nani. Na kwa kufuatana na habari nilizozipata kwa James, hizo karatasi zitabadilishwa kesho usiku.

Jambo jingine ambalo lazima tuchunguze ni mahali ambapo mabadilishano ya karatasi hizo yangefanyika. Kwa kuwa wamekwishajua kuwa tunafanya kazi juu ya jambo hili, wanaweza wakaharakisha mambo zaidi na wakazibadilisha hizo karatasi haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo nasi inatubidi tufanye kazi haraka kusudi tuweze kuzipata hizo karatasi kabla ya wao kuwapa hao watu, na kabla hawajalipwa. 

Haya ndiyo mawzo yangu niliyokuwa nayo. Sammy pia alionekana kuwa na mawazo kama hayo. Tulimpigia Robin simu, tulimweleza juu ya mambo yote tuliyokuwa tunafikiri. Robin alisema, "Ninaona mawazo yenu ni sawa. Walakini inafaa mnipe wasaa maana mimi na vijana wangu tunaanza kupata fununu ya jambo fulani."

Sammy alitoa wazo kuwa yeye ataenda kuchunguza katika ile nyumba ya Benny kama anaweza kupata habari yeyote, kusudi mimi anipe nafasi nilale. Lakini mimi sikukubaliana naye niliona miye ndiye niende, na yeye akiona sirudi, anaweza kuja kunitazama huko. Maana kila siku tunapokuwa tukifanya kazi na Sammy, miye huenda kwanza tukijua ni mahala penye hatari na yeye huja nyuma. Na mara nyingi hii imefanya kuokoa maisha yetu.

Sammy alisisitiza kuwa, kwenda kule peke yangu kunaweza kuwa na maana ya kifo, kwa hiyo ni afadhali twende sote pamoja. Lakini bado niliona hili si sahihi. Mwishowe alikubaliana nami kuwa mimi niende kwanza halafu yeye aje baadaye,baada ya muda kama wa saa moja hivi. 

Nilirudi hotelini kwangu nikabadilisha nguo. Mara hii nilichukua bastola mbili, moja ile yangu ya kawaida, '45 automatic' na ya pili ndogo kiasi cha kalamu ya wino. Hii ya pili niliisukuma kwenye mkunjo wa chupi niliyovaa.

Halafu nikanywa bilauli moja ya maji na whisky. Kisha nikaandika kijikaratasi cha kumwachia Lina, maana nilikuwa namtegemea usiku ule saa sita. Alikuwa amenipigia simu kuwa huenda angalikuwa na jambo kamili ambalo lingeliweza kunisaidia, wakati huo. Ghafla nikajiwa na wazo nimpigie Lina simu, nimweleze kuwa sintokuwepo ila nitaenda kufanya uchunguzi kwenye nyumba ya Benny.

Hii ingenisaidia mambo fulani fulani. Kwanza kama nikimpigia simu Lina, na kama Lina ananicheza yuko upande wa Benyy nitakuta Benny yuko tayari ananingojea maana Lina atamweleza hizi habari. Pili Lina amewahi kuwa mpenzi wa Benny kwa hiyo anafahamu kila kona ya kile chumba. Kwa hiyo anaweza kunipa muhtasari wa jinsi nyumba ilivyojengwa na jinsi vyumba vilivyokaa na hakuna uwezekano wa kufichwa vitu vya siri. Mwanamke..... japo siku moja tu ukikaa naye atakuwa amejua wapi hutaki aende na wapi unataka aende. Basi nilimpigia simu Lina.

"Hallo huyu ni Willy, habari Lina?" 

"Salama tu Willy, mbona unanipigia simu na hali nimekwambia nitakuja? maana mpaka sasa nangojea simu toka mahali fulani ambayo inaweza kukusaidia sana." 

"Oh. unafanya kazi vizuri kabisa Lina. Sababu ya kukupigia simu ni kwamba ninatoka. Naenda kufanya uchunguzi kwenye nyumba ya Benny, kwa hivyo nilitaka unipe muhtasari wa nyumba ilivyokaa, na jinsi ninavyoweza kuingia ndani kwa usalama bila kuzuiliwa."

"Lakini Willy, maahala hapo ni pa hatari sana. Mimi nilipopita karibu na mahali hapo niliona baada ya kuchunguza sana kuwa pamejaa walinzi. Na wote wako tayari kuua mtu yeyote atakayeenda hapo. Miye nilifanya uchunguzi huo nilikuwa huko 'Sclaters hosteli' na niliambiwa hivyo na msichana fulani ambaye ni shemeji ya Benny. Aliniambia kuwa Benny alikuwa amemwambia asiende pale leo maana pana hatari. Na kuwa ingekuwa salama kwake kama angebaki hostelini. Kwa hivyo mimi naona usiende, utahatarisha maisha yako bure tu, tafadhali."

"Hapana Lina, lazima niende. Na wewe njoo kwenye chumba changu ifikapo saa sita hivi. Nadhani bado una ufunguo niliokupa. Wakati huo nina uhakika kuwa nitakuwa nimerudi. Na kama nitakuwa sijarudi jua basi kumetendeka jambo. Sasa nipe huo muhtasari basi."

"Sikiliza Willy, nyumba yenyewe ina vyumba vitano sebule ya sita; choo, bafu na jiko. Vyumba vya kulala vine. Kile cha sita ni namna ya maktaba, maana huwa mna vitabu vingi sana na wageni hawaruhusiwi kuingia humo maana ndipo anatunzia bastola zake na hata za rafiki zake. Nyumba hiyo ina milango mitatu ya nje. Mmoja nyuma kutokea kwa 'Nakuru road'. Upande usio na mlango ni ule wa kulia, ambao unapakana na 'Scrates hosteli,' ila una dirisha moja kubwa la kutosha mtu kuingia kwa dirishani.

Unapoingia utaangukia ndani, utakuwa katika chumba kimoja cha kulala lakini hakina mtu sasa, maana yule shemeji yake ndiye alikuwa akilala humo. Vyumba vyote vya nyuma ni vya kulala. Benny analala kwenye chumba kinachofuata hicho chenye dirisha, mkono wa kushoto wa hicho. Chumba kinachotazamana na mlango wa mbele ukiwa sebuleni, ndicho hicho nilichokueleza, kinachotumiwa kama maktaba. Unataka nikueleze nini tena mpenzi!"

"Hayo yanatosha Lina, asante sana. Kama nikirudi salama ndipo nitaweza kutoa shukrani kwa udhati mbele yako. Hapana shaka tutaonana. Kwa heri mpaka hapo." nilijitengeneza sawasawa, mara hii nilionekana kama mpelelezi haswa mwenye cheti cha kuua.

Nilitoka nje nikaingia ndani ya gari yangu, nikaelekea Westlands. Nilipokuwa ninaenda niliona gari kama mbili zinanifuata kila ninapopita. Nilipofika karibu na 'Klabu 1900' nilisimama. Hizo gari mbili zilikuja zikanipita. Nilipoangalia nikagundua kuwa katika gari la mbele mlikuwa na vijana wawili ambao niliwaacha chumbani kwa Lulu na Benny. Katika gari la nyuma mlikuwa na yule kijana niliyemrudisha wakati akitufuata nilipokuwa na Lina katika gari lake. Nao walienda wakasimama mbele yangu.

Niliwasha gari langu moto nikaenda kulisimamisha na magari mengine hapo klabu 1900. Halafu nikangoja, wale jamaa nao wakaja wakasimamisha magari yao hapo nje kisha wote wakatoka na kuingia klabu 1900. Walidhani mimi nimetoka na kuingia humo, maana nilipokuwa nikizimisha gari langu kijana mmoja naye ndiyo kwanza anawasili hapo, alitoka katika gari lake na kuingia ndani. Alikuwa amevaa koti kama langu, na ni mrefu kama mimi, kwa hiyo walidhani ni mimi. Kisha nilitoka katika gari langu, nikaenda kwenye magari yao, nikapiga risasi magurudumu yote manne ya kila gari, yakawa hayana kazi alafu nikaenda katika hiyo klabu ambamo niliwakuta wote watatu wamekaa huku wakiangaza macho huku na huku. Nilienda nikakaa kwenye meza moja nao alafu nikawaambia,"Tafadhalini wazee, mimi sitaki kufuatwa fuatwa, na kama mkizidi mtaona cha mtema kuni. Mimi nilikuwa nikija hapa kunywa na nyie mnanifuata tu. Sasa nitawaacha hapa, na ninarudi kunywa mjini, na yeyote atakayenifuata nitamwadhiri vibaya sana." kabla hawajajibu niliondoka na kurudi kwenye gari langu. Nililitia moto na kuondoka halafu nikaenda kusimama hatua chache nione kama watatoka. 

Kitambo walitoka, na kuingia katika gari zao. Walipowasha wakakuta magurudumu hayana upepo yote. Walitoka na kuanza kuzungumza. Miye Willy nikaweka gari langu moto, kuendelea na safari yangu. 

Niliondoka hapo kwa mwendo mkali mno. Nilipofika kwenye ile nyumba nikapunguza mwendo. Nikasimamisha gari mbele ya Sclaters hosteli karibu na miti. Hlafu nilianza kurudi kwa miguu, taratibu. Nilikuwa nimeacha koti langu katika gari, halafu nikavaa kijambakoti, ambacho kinanifanya mwepesi zaidi.

Nilienda nikavuka Sclaters hosteli kisha nikaangaza macho yangu mbele ya nyumba hiyo nikaona watu wawili wakizungukazunguka hapo mbele. nikaenda kuchungulia upande wa nyuma pia nikaona kuna walinzi, kama Lina alivyosema. Nyumba yote ilikuwa giza maana hamkuwa na mwangaza hata sebleni. Basi nilikata shauri nifanye kama Lina alivyosema Hapo nikaanza kumsifia Lina kwamba yu mwenye akili hasa. Na kwamba angefaa sana kufanywa mpelelezi.

Nilienda nikaruka seng'enge, nikawa nimeisha anguka ndani ya seng'enge. Lakini mmoja wao alisikia namna ya kishindo kwa hiyo akaja upande ule wangu. Nilijibanza kwenye ukuta. Aliposogea karibu nikamtupia kisu shingoni. Hatimaye mtu huyo alikufa bila mtu kujua. 

Nilipanda mara moja kwenye ukuta, nikakwea taratibu bila kufanya kelele yeyote, mpaka nikashika kwenye dirisha. Hlafu nikatoa tochi yangu na kumulika ndani ya chumba. Nikaona kulikuwa kumelala mtu kwenye kitanda huku ameshikilia bastola mkononi alikuwa amesinzia. Alionekana kana kwamba anataka kuamka lakini kabla ajaamka nilimtia kisu shingoni pia. Akawa hoi bila kutoa sauti. nikaanguka kwenye kitanda bila sauti kutoka kwenye dirisha.

Mlango wa hicho chumba ulikuwa umefunguliwa, kwa hiyo nilitoka nje ya chumba hicho bila kufanya kelele hata kidogo. Nilijaribu mlango wa pili yake ambao Lina alisema ndimo Benny alikuwa akilala, nikakuta umefungwa. Nilichukua funguo yangu malaya nikafungua, nilipopiga tochi mle ndani nikakuta hakuwemo mtu. nilienda kwenye kimeza cha karibu na kitanda, nikaanza kutafutatafuta vijikaratasi vyovyote vya maana lakini sikuona. Ila nilipata karatasi moja ya simu imeandikwa kwa kimombo. 'TELL THE BOSS TO MAKE SURE IT WON'T BE LATER THAN TUESDAY AT 10:00 P.M BECAUSE WE ARE EXPECTING THEM TO LEAVE THAT NIGHT AND BE HERE THE NEXT MORNING.' Fasili yake kwa kiswahili 'umwambie 'BosI' kuhakikisha kuwa Haitazidi jumanne saa nne usiku, maana tunawategemea kuondoka usiku huo na wawe hapa asubuhi ifuatayo" 

Nilitoka kwenye hicho chumba na kufungua mlango nyuma yangu kisha nikaharakisha kwenda sebleni, kutafuta mlango wa maktaba. Maana nilikuwa nafikiRi kama Lina alikuwa anasema kweli, basi huenda humo ndimo mngepatikana mengi. 

Niliingia sebuleni, bahati mbaya nikajigonga kwenye kiti: Yule kijana aliyekuwa mbele ya nyumba alishtuka. Niliweza kumuona sababu mlango ulikuwa wa vioo. Alikaa kidogo huku anaangaza macho ndani, nadhani kwamba alifikiri alikuwa yule mwenzake aliyekuwa amelala mle chumbani, lakini mwishowe alikata shauri ahakikishe, kwa hiyo alifungua mlango.

Mimi nilijibanza kwenye ukuta, alipoingia na kutaka kuwasha taa, nilimmulika na tochi machoni na hapo hapo nikatupa kisu, kikapambana naye kifuani. Kumbe na yeye alikuwa amefyatua bastola yake, na wakati alipoanguka tu, bastola yake ikafyatuka na kutoa sauti.
  
Wale walinzi wawili wa nyuma, walikimbia kwenye mlango wa mbele. Miye nilikuwa tayari nimekwishajibanza na bastola yangu nikiwangoja. Nilisimama kwenye 'swichi' ya taa kusudi wasije wakawahi kuwasha taa. Walipoangalia nje bila kuona lolote, walifungua mlango na kuingia ndani. Mmoja aliyekuwa mbele alitaka kuwasha taa hapo hapo nikaziachia risasi. Bastola yangu ilikuwa na kiwambo kwa hiyo haikutoa sauti. Yule wa nyuma akiwa bado anashangaa pia alizipata risasi.

Mara hii sikuwa na mchezo, madhihaka yote yalikuwa yamekwisha. Nilikuwa nimeishawachukia hawa watu kama kufa, hasa kwa sababu ya mauaji ya John. Kwa hiyo hata mimi sikuwa na huruma hata kidogo. Inaonekana kulikuwa na walinzi kama watano hivi na wote nilikuwa nimewafyeka kabisa.

Nilipiga tochi yangu sebleni, alafu nikakimbia kwenye mlango wa maktaba nikafungua na funguo zangu malaya. Nikaingia ndani halafu nikajifungia na kuanza kupekuapekua. Mlikuwa na vitabu vingi sana. Mlikuwa na masanduku ya vyuma yote yakiwa yamejaa vitabu. Nilifungua kabati moja la chuma, nikaona mlikuwa na bastola kadhaa pamoja na risasi. Pia niliona bahasha moja ambayo ndani yake mlikuwa na barua. Juu yake ilikuwa imeandikwa Dr. Dickisoni Njoroge. 

Nikiwa bado naendelea na upekuzi wangu bila kufanikiwa kupata chochote nilichokuwa nikikitaka, nilisikia mlango wa maktana unafunguliwa. Zilikuwa zimepita dakika kumi. Na nilikuwa nimeweka dakika kumi na tano tu kuwa kwenye nyumba hiyo, kwa hivi zilikuwa zimebaki dakika tano. Na Benny alikuwa ameisha niwahi kabla sijaondoka.

Nilijificha nyuma ya kabati hilo la chuma. Alipofungua aliwasha taa, hakuwa Benny ila kijana mwingine. Aliangaza huku na huko bila kuniona. Lakini mwishowe niliona akija upande wangu. Nilitoa kisu changu, kabla hajageuka, nikampata mgongoni, akaanguka bila hata yowe! Nilikimbia mlangoni. Nikaangaza sebuleni ambamo sasa taa zilikuwa. Sikuona mtu, nikakimbia mpaka kwenye mlango wa mbele, kabla sijatoka nje, nilipigwa kichwani mpaka chini. 

Nilipozinduka nilijikuta nimefungwa kitini! Karibu yangu alikuwa Sammy pia amefungiwa kitini huku bado amezimia! Benny na Lulu walikuwa wamesimama karibu nami huku wakionekana na furaha sana. 

"Naamini muda huu huna ujanja Willy, ninakuhurumia sana, maana kifo chako pamoja na rafiki yako kitakuwa kibaya na cha maumivu sana. Nami nitahakikisha kuwa mmekufa kwa taabu maana nyie mnaonekana watu wa ajabu sana, kumbe mambo yote waliyoandika juu yako ni kweli".

"Wewe umeniingiza hasara sana ya watu wangu, maana umeua sita, na huyu rafiki yako ameua watano wakati akijaribu kuja kukuokoa lakini na yeye ameangukia kwenye mkasa huo huo." Alisema kwa kujivuna sana.

"Sasa unadhani utafaulu kwenye mipango yako eti?"

"Kwanini nisifaulu, mpaka sasa yote yamekwisha kamilika, ila wewe tu na huyu rafiki yako ndiyo mlikuwa mnanipa taabu, lakini sasa hamtanipa taabu tena. Na sasa watu wangu wote watafanya sikukuu wakisikia wewe, John, na huyu anayeitwa Sammy amekufa".

"Umefahamje kuwa huyu ni Sammy?"

"Lo! Wewe ndiye umechelewa kweli, nimekwambia saa zile kuwa kikundi chetu hata polisi wenyewe wamo. Nitashindwaje kujua basi. Nyie kila siku mnadhani ndiye wenye kujua habari nyingi, lakini mimi nina habari nyingi zaidi yenu, na ninatumia akili zangu zaidi yenu nyie. Na pia nahakikisha kuwa sifanyi kosa hata moja".

"Hii mipango mmeianza lini, na nani aliwasaidia katika jambo hili maana nyinyi msingelijua wapi pa uhakika ziliwekwa hizo karatasi?"

"Bosi' aliniambia kwamba nisiwaeleze jambo lolote mpaka amri itakapotoka kwake, lakini kwa sababu miye sitaki kuwaona mnaishi tena, nimeleta madebe mawili ya 'Petrol' na vijana wangu watawamwagia na kuwawasha moto mpaka mtakapokuwa mmeungua na kubaki majivu."

"Unafurahi, kuchoma watu eh Benny, lakini kabla sijamalizika kabisa wakati nikiungua na wewe utakuwa umekufa." Nilijibu kwa dhihaka.

"Uh, unadhani natania, Amani. Lete hayo madebe ya 'Petrol' pamoja na kiberiti," aliita kwa hasira.


Wakati huo Sammy alikuwa ameisha zinduka akasema, "Wewe shetani mwanamke, siku moja nitakata kipande cha nyama katika mwili wako na kukifanyia sikukuu."

"Nyamaza mwehu we, utaikataja nyama yangu na hali utakuwa umeisha kufa?" Alisema huku akitabasamu.

"Naona hapa tutakufa kama wanawake Willy, lakini hata hivyo huyu mwehu atashikwa na kutiwa ndani, nitafurahi sana kumpokea huko chini, na lazima nitahakikisha kuwa atapata taabu mpaka kupata makao," alisema Sammy huku akionekana hajali lolote. Benny alitoa kicheko. Halafu akamwambia Aman atumwagie petrol.

Kabla hajamwaga Lulu alitoa oni, "Nadhani 'Bosi' atapenda kuwaona hawa washenzi wakiungua, kwa hiyo afadhali tumfuate aje ajionee hawa watu mashuhuri wa Serikali wakifa kitoto, na kifo cha aibu. Unaonaje Benny?"

"Lakini lazima tuache ulinzi wa kutosha hasa. Mlango wa nyuma weka walinzi watatu. Huu wa mbele watatu. Na wengine kuzunguka nyumba, halafu kwenye mlango wa chumba hiki watatu pia. Naamini hata kama angekuwa malaika hawezi kutoroka kwenye ulinzi wa namna hii."

Wazo wako ni zuri sana Lulu. Nadhani 'Bosi' atafurahi ajabu na atatufanyia sikukuu. Lakini nyie wote angalieni kuwa hamfanyi kosa hata kidogo. Kosa lolote mshahara wake ni kifo cha namna hii hii.

Nilimuuliza mlinzi mmoja aliyekuwa akifunga mlango wa chumba tulichokuwa, "Itawachukua muda gani kwenda kwa 'Bosi' na kurudi?"

"Kama dakika kumi hivi". alijibu na kisha akatufungia ndani. Halafu wakasimama pale mlangoni hali walinzi watatu wakiwa tayari na silaha zao. 

Tulikuwa tumefungwa sana, hivyo kwamba hatukuweza hata kujitingisha. Walikuwa wametuvua nguo zetu zote isipokuwa chupi tu ajabu ni kwamba niliweza kusikia bado bastola yangu ndogo imo kwenye mikunjo ya chupi yangu. Jinsi ya kuitumia ilikuwa haifahamiki hata kidogo. Kuwa nayo na kutokuwa nayo yote yalikuwa mamoja. Na pia tulijua tungefanya upuuzi wowote kabla Benbny, Lulu na 'Bosi' hawajarudi tungeliteswa na hawa walinzi. 

"Mara hii hatuna ujanja kweli Sammy."

"Hata mimi naona, maana sidhani kwamba kunaweza kuja mtu wa kutuokoa, na kama pia atakuja atakufa kabla hajafika humu ndani!"

"Mie nilikuwa siku zote natabiri kufa kwa risasi, maana pia nimeisha ua wengi kwa risasi".

"Hakuna njia Willy, ila huenda mizimu ya mama Sammy ifanye kazi yake. Unakumbuka tulivyopona safari ile kule Lusaka?"

"Ndiyo, nakumbuka, lakini ulinzi pale haukuwa mkali kama huu wa hapa".

Mawazo yangu yalirudi Dar es Salaam. Nilimfikiria mpenzi Della, moyo ukaniuma namna ya ajabu. Nilijua Della angeweza kujiua kama angesikia nimekufa. Nilimpenda naye alinipenda. Alikuwa msichana wa peke yake aliyechukua moyo wangu na ambaye nilichukua moyo wake. Kisha nikamfikiria mama Willy. Lo! Mimi nilikuwa mtoto wake wa pekee. Hakuwa na mtoto mwingine hata mmoja. Mama Willy nilijua atakapoambiwa tu, ataanguka chini na kufa. Nilijua jinsi mama alivyokuwa akinipenda. 

Nilionekana kama mawazo yangu si sawa. Nilikuwa katibu nipate kichaa kwa kufikiri mambo kama haya. Kisha nilimsikia Sammy akisema, "Nimesikia kitu kama mlio wa bastola yenye kiwambo!.

"Unaota nini Sammy".

"Hapana, kweli nimesikia." Kisha nami nilisikia kishindo kwenye mlango kana kwamba watu wanaanguka. 

Mwishowe nilimwambia Sammy kuwa huenda ni 'Bosi' anafika kwa hiyo watu wanamtolea njia. 

Tulisikia mlango wa chumba ukifunguliwa. Moyo wangu uliruka kwani nilijua sasa mwisho wetu umefika. Maana "Bosi" amafika. Nilipomtaza Sammy niliona nywele zake zikisimama na rangi ilibadilika. "Wameisharudi! Alisema. 

Mlango ulipofunguliwa tulishtuka kuona ni Lina ndiye anafungua mlango. Alikuwa ameshika bastola mbili mkononi. Akazitupa chini akaja kunifungua. "Harakisheni tutoke hapa mapema kabla hawajarudi, maana nasikia watarudi mnamo dakika mbili au moja unusu hivi."

ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU