NGUVU YA RUSWA
II
Willy Gamba
akifuatana na Bibiane usiku huo, huku mkononi mwake ameshika bunduki kubwa aina
ya AK 47, walitembea kwa tahadhari kubwa kuelekea nyumbani kwa Col. Rwivanga.
Walipofika hawakumkuta na nyumba yake ikiwa imefungwa. Kwa vile Willy alikuwa
amepewa ufunguo wa ziada, walikuwa wameamua kwa ajili ya swala la kiusalama
Willy awe analala pale, Alifungua mlango na kumvuta Bibiane ndani. Aliwasha taa
ya sebuleni na kumsukumia Bibiane kwenye kochi.
Kwa mara ya
kwanza ndipo Willy alipomwangalia Bibiane vizuri. Alistaajabu kuona kiumbe
kizuri kama hiki kilivyojiingiza kwenye vitendo vya ugaidi wa ajabu. Hakika
huyu msichana alikuwa mzuri. Ukisikia mrembo, urembo hio huu. Willy katika
maisha yake alishawaona wasichana warembo lakini huyu alikuwa msichana mrembo
kwelikweli.
"Asante
kwa kuniokoa", Bibiane alimshukuru Willy Gamba huku akiwa amelegeza macho
yake na kuonyesha tabasamu la aina yake mbele ya Willy ambaye alikaa kimya
akimwangalia bila kujibu.
"Sasa
niko upande wako, usipate taabu kunilinda, kwa jinsi ulivyookoa maisha yangu
sasa nifanye vyovyote upendavyo", Willy kwa kumwangalia Bibiane machoni
aliamini kuwa anasema ukweli.
"Nenda
kaoge", Willy alimweleza Bibiane huku akielekea kwenye chumba alichokuwa
akilala. Bibiane aliinuka taratibu na kumfuata Willy. Chumba alichokuwa akilala
kilikuwa na maliwato ya ndani. Hivyo, alimuonyesha ishara Bibiane alifungua
mlango na kuingia ndani.
Wakati
Bibiane anaoga, Willy aliingia jikoni na kutayarisha kahawa. Alipoangalia saa
yake ilikuwa yapata usiku wa manane. Alishangaa kwa nini Col. Rwivanga alikuwa
hajarejea, akajiuliza ameelekea wapi
wakati huo.
ITAENDELEA 0784296253
tuko pamoja kaka mpaka mwisho
ReplyDelete